MGEJA AWALIPUA WANASIASA WANAOSHINIKIZA IGP SIMON SIRRO AJIUZULU



Mwenyekiti wa Taasisi ya Tanzania Mzalendo Foundation Khamis Mgeja

****
Na Baltazar Mashaka - Mwanza

BAADHI ya Viongozi wa vyama vya upinzani, wanasiasa na wanaharakati wanaoshinikiza Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP) Simon Sirro, kujiuzuku kwa madai ya kuzuia mikutano ya kisiasa ya ndani na ya hadhara, wamuache atekeleze majukumu yake bila kuingiliwa.


Rai hiyo imetolewa leo na Mwenyekiti wa Tanzania Mzalendo Foundation,Khamis Mgeja,kwenye Hoteli ya Rock Beach jijini Mwanza,wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mustakabali wa nchi pamoja na mambo mengine.

Alisema kauli za baadhi ya viongozi wa vyama vya upinzani,wanasiasa na wanaharakati,wanaoshinikiza IGP Sirro kujiuzulu wadhifa huo kwa madai ya kuzuia mikutano ya ndani na ya hadhara ya vyama vyao, wamekosa hoja ya msingi,hivyo Watanzania wanapaswa kuwapuuza.


Mgeja ambaye yupo jijini Mwanza kwa mapumziko mafupi alisema, kauli zilizotolewa hivi karibuni na baadhi ya wanasiasa,wakimtaka IGP Sirro kuachia wadhifa huo, hazina chembe ya uungwana,adabu na heshima kwa mkuu huyo wa jeshi la polisi.

Aliwaelimisha wanasiasa hao wakiwemo Watanzania wanaomtaka Sirro,kujiuzulu watambue kazi kubwa inayofanywa na jeshi la polisi na vyombo vingine vya usalama, ni kwa maslahi mapana ya nchi katika kuimarisha ulinzi na usalama wa raia na mali zao.

Pia ulinzi unagusa masuala ya uchumi wa nchi,yakiwemo maendeleo, utalii,uwekezaji na wafadhili wanaotufadhili bila usalama unaosimamiwa na jeshi la polisi chini ya IGP na vyombo vingine,vikitetereka yote hayawezi kupatikana wala kufanyika na watalii hawawezi kuja.

Mwenyekiti huyo mstaafu wa CCM Mkoa wa Shinyanga, alisema utendaji kazi wa IGP hauwezi kupimwa kwa kuruhusu ama kuzuia mikutano ya ndani na ya hadhara ya vyama vya siasa hasa ya baadhi ya viongozi wa vyama vya upinzani,wanasiasa na wanaharakati.

“IGP ana majukumu mengi na nyeti kila siku kuhakikisha nchi inakuwa salama na usalama wa raia na mali zao, kwa hilo hatuna mashaka nalo, nchi iko shwari watu wanaendelea kuchapa kazi ya kulijenga taifa,haiingii akilini kwa raia wema wanaoitakia mema Tanzania wamtake IGP aachie ngazi kisa mikutano ya kisiasa imezuiwa,”alishangaa Mgeja.

Aliongeza kuwa Kamanda Sirro na jeshi la polisi wanastahili kupongezwa kwa namna wanavyohaingaka nchi nzima kuhakikisha Watanzania wanakuwa salama na mali zao wakiwemo hao wanaoshinikiza ajiuzulu, jeuri hiyo wanaipata kwa kuwa wananufaika na utendaji wake.

“Nitoe rai kwa viongozi wa vyama vya siasa, inapotokea mikutano yao kuzuiwa kwa sababu za usalama,ni vyema wakawa na subira na utii wa sheria bila shuruti, inawezekana ni wao wenyewe na hasa viashiria vya uvunjifu wa amani,nchi zingine tumeshuhudia wakipigana kwa kurushiana viti ama kutega mabomu ukumbini,”alisema Mgeja.

Alisisitiza jeshi la polisi lina njia nyingi za kupata taarifa za kiintelejensia na kwa kazi nzuri inayofanywa na Polisi chini ya IGP Sirro,wamuache na askari wake wafanye kazi kwa uhuru bila shinikizo wakiongozwa na miongozo ya jeshi la polisi.

Aidha Mwenyekiti huyo wa Tanzania Mzalendo Foundation inayojihusisha na masuala ya demokrasia,haki za binadamu na utawala bora, alisema Watanzania wajenge utamaduni wa kupongeza watendaji wa umma wanapofanya kazi nzuri ili kuwatia moyo, wawe na ari ya kufanya kazi kwa bidii.

“Hawa wanaomtaka Sirro ajiuzulu hawana chembe ya shukrani,yaani hakuna jema hata moja alilofanya la kupambana na uhalifu ili kuwafanya wananchi na wana siasa walale usingizi wa pono, ifike mahali washukuru na huo ndio uungwana badala ya kuangalia eneo moja tu,” alishauri.

Mgeja alieleza watu wafahamu kazi ya jeshi la polisi ni kulinda usalama wa raia na mali zao,kazi ambayo ni ngumu, unapotokea uhalifu au madhara wanalaumiwa wao je,wanasiasa hao hawazioni kazi hizo na kama sivyo wamuache IGP afanye kazi na utendaji wake haupimwi kwa kuruhusu mikutano ya ndani na ya hadhara ya vyama vya siasa.

Alidai jeshi la polisi haliwezi kubebeshwa lawama kwa kosa la askari mmoja, ni sawa na muumini mmoja akikosea kanisa au msikiti hauwezi kulaumiwa kwa makosa ya muumini huyo.

Mgeja aliiomba jamii, wanasiasa na wanaharakati kukubali ukweli wanapokosolewa na kuelimishwa, wasilalamike na kukimbilia kulaumu kuwa IGP anakiuka haki za binadamu, hivyo waendelea kutoa ushirikiano kwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan, pia jeshi la polisi chini ya IGP Sirro.

“Tusikimbilie kulalamika IGP anakiuka haki za binadamu,ni mambo ya ajabu watu kukataa kukosolewa na kuelimishwa na tutakuwa taifa la watu wa ajabu sana, tusifike huko, tuendelee kumsikiliza na kumuunga mkono kwa dhati Sirro anavyoelimisha jamii, kusimamia utendaji wa askari na maofisa wa polisi, kufanyia kazi changamoto za usalama wa nchi ili kila raia aisha kwa amani,”alisistiza.

Pia alitumia fursa hiyo kuiasa jamii na wazazi kutimiza wajibu wao wa malezi ya watoto katika kuandaa kizazi kijacho na kuwajenga wawe raia wema, kwa sababu wazazi ndio wanaokaa na watoto,wakiharibika watalaumiwa kwa malezi mabaya.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments