SPIKA JOB NDUGAI : TOZO ZA MIAMALA YA SIMU NI HALALI,...UNAYEPINGA TUPE NJIA MBADALA TUTAPATA WAPI FEDHA


Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Ndugai

Na Dotto Kwilasa, Dodoma.

Baada ya mijadala mingi kuhusiana na tozo ya miamala ya simu hususani kwenye mitandao ya kijamii ,Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Ndugai ameibuka na kudai kuwa tozo hizo ni halali na kwamba fedha hizo zitachagiza masuala ya maendeleo ikiwemo huduma za kijamii kama vile shule,hospitali na maji.

Hatua hiyo imekuja kufuatia baadhi ya wananchi kulalamika kwamba kumekuwa na tozo kubwa katika miamala ya simu huku akipigilia msumari kwenye tozo hizo kwa kudai kuwa Bunge ndio limepitisha na kwamba wanaopinga wanatakiwa kutoa mawazo mbadala nini kifanyike huku akisisitiza lengo ni ifikapo 2025 Tanzania iwe Taifa tofauti katika suala la Maendeleo.

Akizungumza mapema leo Julai 23,2021,katika kikao kazi kilichoandaliwa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma,Anthony Mtaka,Spika Ndugai amesema "Sisi kama Bunge tulikaa kwa pamoja na kujadiliana kisha tukaamua kuwa na tozo katika miamala ya simu kwa sababu fedha zitakazopatikana zitaenda katika mfuko Maalum ambao utawasaidia wananchi,"amesema na kuongeza;


"Tumepitisha na tukatunga sheria , tunataka kuliona hilo,sasa wewe ambaye unapinga tupe njia mbadala tutapata wapi fedha, tunafikaje 2025, kwa hiyo maamuzi ni hayo tumeyafanya, kwa nia njema kabisa kwamba 2025 tuwe tumetoka, tuwe ni taifa la Tanzania ambalo ni tofaut,CCM hoyee,nimemaliza,"amesema Spika huyo.


Pamoja na hayo amezungumzia kuhusu maendeleo ya mkoa wa Dodoma na kuwataka watendaji wa mkoa wa huu kujitathimini katika utekelezaji wa majukumu yao kwani serikali imekuwa ikitimiza wajibu wake kwa kuleta fedha kwa wakati lakini tatizo lipo kwa watendaji.

"Naomba nitolee mfano kwa mkuu wa mkoa wa huu Antony Mtaka ,alimetoka Simuyu kule alifanya kazi nzuri, hivyo hapa akishindwa kufanya vizuri tujue kabisa tatizo lipo kwetu na sio kwake,tukishirikiana nae vizuri ataacha alama kubwa kwenye Mkoa wetu,"amesisitiza Ndugai.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Anthony Mtaka amebainisha vipaumbele vinne ambavyo atavisimamia katika mkoa wa Dodoma na kusema kuwa kama watafanikiwa, Jiji la Dodoma litakuwa la kiuchúmi zaidi.

Amevitaja vipaumbele hivyo kuwa ni pamoja na Elimu, migigoro ya Ardhi, kilimo na ufugaji venye tija na huduma bora za sekta za afya huku akitangaza alizeti kuwa zao la biashara katika mkoa huo.

Akizungumzia katika kikao hicho ametaja lengo la kikao hicho kuwa ni kuweka mikakati ya pamoja ili kwenda pamoja kama timu katika kutekeleza mambo yanayohusu maendeleo.

"Ukitaka kufanikiwa nenda na wenzako,nawasii tuwe na lugha ya pamoja yapo Mambo mazuri wenzetu wameyafanya hivyo lazima tuyaendeleze, sisi Dodoma tunautofauti tunabeba haiba ya makao makuu ya nchi hivyo ni lazima tuwe na matarajio makubwa,"amesema.

Licha ya hayo Mtaka amezungumzia kiwango cha elimu Mkoa wa Dodoma kuwa kipo katika hali mbaya, katika ngazi zote ikiwemo mitihani ya mock kwa mkoa haujafanya vizuri hivyo zinahitajika nguvu za ziada kuhakikisha mkoa unafanya vizuri katika sekta ya elimu na kuondokana na aibu iliyopo.

"Halmashauri zote nane za mkoa wa Dodoma mnatakiwa kuwa na ubunifu wa vyanzo vipya vya mapato ambavyo vitatuingizia fedha za kutosha kuendesha miradi mbalimbali,na kuufanya Mkoa wetu kuwa wa mfano,"amesisitiza Mtaka.

Amesema Jiji la Dodoma limekusanya sh.bilioni 70 kutokana na mauzo ya viwanja sasa wapo kiwango cha sh.bilioni 30 hivyo lazima watafute vyanzo vipya vya mapato na anatamani kuona ubunifu katika suala hilo.

"Natamani kuona kila kaya zikipanda miti mingi kwa ajili ya Utunzaji wa mazingira pamoja na kuweka Mipango mizuri ya Utunzaji wa mazingira katika mkoa huu,"amesemà.

Mtaka pia amesisitiza kuwa "Lazima niseme ukweli kwamba ili tufanikiwe Katika yote haya tuukatae uchonganishi na unafki,Wapo Watumishi waongo na wachonganishi siwapendi, watu wanachonganisha watu, hasa Halmashauri ya Wilaya ya Kondoa, tumekutanishwa na kazi tufanye kazi tuheshimiane kiongozi haongozwi,".

Akitilia mkazo suala hilo amesemà ikitikea watumishe waongo na wachonganishi wakiendelwa kumtumia meseji atawataja hadharani ili kuepusha maneno na vikwazo katika uongozi wake.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments