HESLB YAMPONGEZA RAIS SAMIA ONGEZEKO LA BAJETI YA MIKOPO

Na Mwandishi Wetu,
BODI ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imempongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa hatua ya Serikali kuongeza bajeti ya Mikopo ya Elimu ya Juu kwa mwaka wa masomo 2021/2022 yenye kiasi cha TZS 570 Bilioni iliyoweka historia katika taasisi hiyo.

Akizungumza wakati wa hafla ya kufunga Maonesho ya 16 ya Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia Jijini Dar es Salaam leo Jumamosi tarehe 31 Julai, mwaka huu Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB, Abdul-Razaq Badru alisema ongezeko la bajeti hiyo ni kielelezo cha dhamira ya dhati ya Serikali ya kusaidia Watanzania wahitaji.

Badru alisema katika bajeti hiyo yenye uwezo wa kusomesha wanafunzi 160,000, imewalenga wanafunzi wahitaji wanaotokea katika kaya zisizojiweza na hivyo kuwataka kuhakikisha kuwa wanakamilisha taratibu za maombi kama zilivyoanishwa katika mwongozo wa uombaji mikopo wa mwaka 2021/2022.

Kwa mwaka jana bajeti yetu ilisomesha wanafunzi 55,000 wa mwaka wa kwanza na kwa mwaka huu tunaratajia kusomesha wanafunzi 62,000 hii ni idadi kubwa kwa mwaka huu, tunawaomba wanafunzi wahitaji kuhakikisha wanaomba kwa usahihi” alisema Badru.

Akizungumzia kuhusu hali ya urejeshaji Mikopo, Badru alisema kwa sasa kumekuwa na mwitikio mkubwa kwa wanafunzi wanufaika kurejesha mikopo yao kwa hiari, hatua iliyotokana na Serikali kufuta tozo na adhabu mbalimbali zilizokuwepo awali.

Kuanzia Mwezi Julai mwaka huu, kumekuwa na ongezeko kubwa la wanafunzi wanufaika kurejesha mikopo yao, na hapa katika maonesho tumeshuhudia wanufaika wengi wakifika katika Banda kwa ajili ya kupata taarifa za madeni ya mikopo” alisema Badru.

Aidha Badru alisema HESLB itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo waajiri ili kuhakikisha kuwa madeni ya mikopo kutoka kwa wanafunzi wanufaika inarejesha ili kuiwezesha Serikali kuwa na Mfuko endelevu.

BONYEZA HAPA KUJUA VITUO VITAKAVYOTOA CHANJO YA CORONA TANZANIA



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments