RAIS SAMIA KUUNDA TIMU YA WATAALAMU KUFUATILIA KUHUSU CORONA


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akihutubia mara baada ya kuwaapisha MAkatibu Wakuu, Naibu Makatibu Wakuu na Wakuu wa Taasisi Ikulu jijini Dar es salaam leo Jumanne Aprili 6, 2021
***
Na Said Mwishehe, Michuzi TV.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amesema anatarajia kuunda timu ya watalaam ambao watafuatilia kwa kina kuhusu janga la Corona na kisha kutoa kuishauri Serikali nini kifanyike na kama tunakubali au tunakataa kuhusu Corona basi ifahamike badala ya kukaa kimya.

Amesema hayo leo Aprili 6 mwaka 2021 wakati akihutubia Taifa baada ya kuwaapisha makatibu wakuu na manaibu makatibu wakuu wa Wizara mbalimbali ambao wamepa baada ya kuteuliwa Aprili 4 mwaka huu ambapo pamoja na mambo mengine ameweka wazi katika janga la Corona kuna haja ya kupata maoni ya washauri kupitia timu ya watalaamu ambayo ataiunda kufanya tafiti wa kina.

"Katika hili la COVID natarajia kuunda kamati kwa ajili ya kufanyika tafiti ya kitalaam, watuambie upeo hayo yanayosemwa , hatuwezi kupokea kila kinacholetwa, Rais Kikwete aliwahi kutuambia akili za kuambiwa changanya na za kwako, lazima kwenye COVID tueleweke kama tunakubali au tunakataa,"amesema Rais Samia.

Wakati huo huo, Rais Samia mbali ya kuzungumzia COVID na mkakati wake wa timu ya watalaamu, amezungumzia bima ya afya kwa wote ambapo amesema watalaam wamalize mchakato na wapeleke serikalini ili wajadiliane kwa pamoja. "Kuna mambo hapo katikati kwenye bima, kasimamieni suala la bima, watanzania wanakata bima za afya lakini wakifika kule hakuna dawa".

Aidha amezungumzia changamoto ya ukosefu wa dawa ambapo ameitaka Wizara ya Afya kuhakikisha inashughulikia hiyo changamoto kwani kwenye Wilaya na Mikoa kuna upungufu mkubwa wa dawa."Tukatazame tatizo liko wapi, najua dawa zinapotea hapo katikati, tukaondoe hili tatizo".

Ametumia nafasi hiyo kusisitiza umuhimu wa watumishi kufanya kazi kwani Serikali yake ni kazi tu na kwamba wakati ule ni ule tu na umeshapita."Hapa tufanye kazi tu , mkasimamie utekelezaji wa Ilani ya CCM ili wote tuweze kurudi tena.

"Mkienda kubabaisha Ilani, wananchi nao wana maamuzi yao, tunajua utekelezaji huu unahitaji fedha na ubunifu,mkiwa wabunifu mtatekeleza mambo mengi tu.Nina matarajio makubwa na watendaji waliopo serikalini, tufanye kazi."

CHANZO - MICHUZI BLOG

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments