TARI NALIENDELE KUONGEZA UZALISHAJI WA ZAO LA KOROSHO MKOANI RUKWA

 


Na. Abdulrahman Salim
Afisa Habari Ofisi ya Mkuu wa Mkoa – Rukwa.
Bodi ya Korosho Tanzania kwa ushirikiano na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) kituo cha Naliendele Mkoani Mtwara Imemkabidhi Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo kilo 400 za mbegu za korosho ili aweze kuzigawa kwa Wakuu wa Wilaya na hatimae kuwafikia wakulima kupitia Maafisa kilimo wa halmashauri za mkoa huo.  

Akizungumza kwa niaba ya Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Korosho Tanzania wakati wa kukabidhi mbegu hizo Kaimu meneja wa mipango ya kilimo wa Bodi hiyo Juma Yusuf alisema kuwa wamekabidhi mbegu hizo kwa uongozi wa mkoa kwa lengo la kuanzisha mashamba darasa kwenye maeneo ya halmashauri zilizoteuliwa kwaajili ya kilimo cha zao hilo.

Alisema kuwa mbegu hiyo mseto ni miongoni mwa aina za mbegu 54 zilizo bora zinazozalishwa na TARI Naliendele na kuongeza kuwa korosho inayotokana na mti wa mbegu hiyo sio kwaajili ya matumizi ya kuzalisha mbegu nyingine bali ni kwaajili ya ulaji tu na kuongeza kuwa unaweza kutumia vikonyo vya miche inayotokana na mbegu hiyo kwaajili ya ubebeshaji kwenye mbegu yoyote ya mkorosho wa asili na kusababisha mkorosho nao ukawa bora.

Akielezea faida za mkorosho unaotoka na mbegu hizo Yusuf alisema kuwa endapo mbegu hizo kilo 400 zitapandwa kwa kufuata maelekezo na kanuni za kilimo na endapo haitaathiriwa na chochote kuna uwezekano wa kupata Shilingi Bilioni 3.4 baada ya miaka nane ijayo.

“Kwasababu hii ni mbegu mseto na ni mbegu bora, inaanza kutoa mazao kwa maana ya korosho ni baada ya miaka miwili lakini haziwi nyingi za kutosha lakini itakapofikia miaka minane itaanza kutoa zile korosho za kutosha kama itakuwa imetunzwa vizuri nah apo kwa mkorosho mmoja unaweza kutoa kwa wastani kilo 15 hadi 25 kwa kusema hivyo ekari moja itakuwa na miche 28 yenye wastani wa uwezo wa kutoa kilo 600, kwa mbegu hizi kilo 400 zinatosha kwenye ekari 2,000 itakayokuwa na mikorosho 56,000 ikienda vizuri tunaweza kupata kilo milioni 1.4 ya thamani ya Sh. Bil 3.2,”Alisema.

Kwa upande wake Mh. Wangabo alisema kuwa awali alisikitishwa baada ya kusikia kuwa zao la korosho linafaa Zaidi kupandwa mkoani Katavi na hivyo kuwaomba wataalamu wa TARI naliendele wafanye utafiti mkoani Rukwa ili kuona uwezekano wa kuwa na zao hilo na hatimae utafiti umeonyesha kuwa zao hilo linaweza kupandwa katika ukanda wa bonde la ziwa Rukwa Wilayani Sumbawanga Pamoja na baadhi ya maeneo katika Wilaya za kalambo na Nkasi.

Aidha alisema kuwa katika kipindi cha miaka kitatu iliyopita Mkoa wa Rukwa umefanya juhudi mbalimbali za kuhamasisha wananchi kupanda mazao mbadala na mahindi ikiwemo kupanda maparachichi, kahawa, michikichi Pamoja na Korosho ili wananchi wawe na mazao mengi ambayo yanaweza yakawasaidia kupata kipato kuliko kutegemea zao la mahindi pekee.

“Nitoe wito kwa wananchi na wakulima wa mkoa wa Rukwa kwa ujumla wachangamkie hii fursa, haya maeneo ambayo nimeyataja, maeneo ambayo kama yanastawi korosho, wapande korosho kama hizi hapa korosho bora kabisa, kwahiyo watu wa Rukwa tuchangamkie fursa hizi kwahiyo panda mikorosho, panda parachichi, panda kahawa, panda zao lolote lile ambalo unaona linafaa ilimradi tutoke katika uchumi ule tuliouzoea wa mazao yale ya chakula kuwa mazao ya biashara kwahiyo tuyalime yale kama mazao ya chakula na ziada ya haya maalum kwaajili ya biashara,” Alisisitiza.

Kilo hizo 400 zimegaiwa kwa halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga ambao wapewa kilo 150 kwaajili ya ekari 42 zilizotayari kwaajili ya kupanda, Halmshauri ya Wilaya ya Nkasi wamepewa kilo 125 kwaajili ya kuwapatia wakulima 172 waliotayari kulima zao hilo Pamoja na kilo 125 wamepewa Halmshauri ya Wilaya ya Kalambo.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments