MWANAMKE AMWAGIWA CHAI YA MOTO AKIDAI TALAKA KWA MME MWENYE MCHEPUKO

Zikiwa zimepita siku kadhaa tangu dunia ihitimishe siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia, Mariam Msafiri amemaliza mwaka vibaya kufuatia majeraha makubwa yaliyotokana na kumwagiwa chai ya moto na mumewe.

Mariam (25) mkazi wa Mbande Kisewe na mama wa watoto watatu, alikumbwa na kadhia hiyo asubuhi ya Desemba 17 mwaka huu wakati akiandaa chai kwa ajili ya kifungua kinywa cha familia yake.

Akizungumza na Mwananchi Mariam alieleza kuwa kabla ya tukio hilo mara kadhaa amekuwa na migogoro na mume wake aliyemtaja kwa jina la Seif Abdul lakini siku hiyo alifikia hatua ya kumwagia chai iliyokuwa inachemka jikoni.

Anasema, “Kabla ya siku hiyo tulikuwa na ugomvi chanzo ni kwamba ana mwanamke mwingine na nikamwambia kama vipi anipatie talaka ili tuachane kwa usalama, akanipeleka hadi kwao kwa madai anakwenda kunikabidhi talaka yangu lakini hakufanya hivyo akaniacha huko, akatokomea.’’

Aliongeza: ‘‘Kwa kuwa nyumbani kwao na tunapoishi sio mbali ,nilirudi nyumbani kwangu nikalala na watoto wangu, yeye hakurudi siku hiyo. Asubuhi nikaamka kuendelea na shughuli zangu kama kawaida ikiwamo kuandaa kifungua kinywa. Nilibandika chai kwenye jiko la gesi.’’

Mariam alisema kuwa mumewe alirejea asubuhi hiyo wakaanza mizozo tena, ndipo alipomtamkia wazi kwamba yuko tayari kumuacha ila lazima amuachie kilema.

“Aliponiambia hivyo ndipo akachukua ile chai iliyokuwa jikoni lengo lake animwagie usoni, niliwahi kukinga mkono ikasaidia kuzuia isiende usoni; matokeo yake nikaungua kwenye mkono wa kushoto kama hivi unavyouona.’’

Via Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments