WIZARA YA AFYA YASEMA IMEJIPANGA KUTOA ELIMU YA BIMA YA AFYA KWA WOTE


Na. Catherine Sungura, WAMJW- Dar es salaam
Katika kuelekea kwenye bima ya afya kwa wote, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imejipanga kutoa elimu kwa jamii ili wananchi waweze kuelewa umuhimu wa kuwa na bima kuliko kusubiri hadi pale watakapougua.

Hayo yamesemwa leo na Prof. Mabula Mchembe, Katibu Mkuu Wizara ya Afya wakati wa siku ya pili ya kongamano la kitaifa la kisayansi la magonjwa yasiambukiza linaloendelea jijini hapa.

Prof. Mchembe amesema hivi sasa huduma za afya kuazia ngazi ya zahanati hadi hospitali za taifa huduma za afya kwenye miundo mbinu,vifaa na vifaa tiba zimeboreshwa hivyo kwa kuwa na bima ya afya kwa wote itasaidia kupata huduma nzuri zaidi.

“Serikali kupitia Wizara ya Afya hivi sasa inatoa huduma za afya bila malipo kwa watoto chini ya miaka mitano,wazee na wale wenye saratani katika huduma za matibabu, dawa na huduma zingine,hivyo tunahitaji kuboresha zaidi vituo vyetu vya afya ,vifaa pamoja na watumishi ili kuweza kutoa huduma bora zaidi”.

Hata hivyo Katibu Mkuu huyo amewataka wale wenye bima ya afya ya NHIF waweze kujenga mazoea ya kulipa kidogo kidogo kila mwezi ili inapofika mwisho wa mwaka wawe wamekamilisha na hivyo itasaidia kutokwama kwa malipo ya awamu nyingine pale kadi inapomaliza muda wake.

Kwa upande wa magonjwa yasiyoambukiza amesema kuwa wizara pamoja na taasisi zake zote zinahusika katika kuzuia na kukinga mangonjwa yasiyoambukiza, hivyo amesisitza wananchi kuwa waangalifu kwenye vyakula pamoja na kuacha matumizi holela ya dawa.

“Watu wengine wanatumia dawa holela na ambazo zimeisha muda wake au kwa kutoandikiwa na wataalam,tuhakikishe tunatumia dawa zenye ubora kwani kila dawa ina madhara yake hivyo dawa zitumike kufuatana na malengo tarajiwa. Sisi kama wizara tutatumia wataalam wetu kuwaelimisha wananchi matumizi sahihi ya dawa.

Naye Mkurugenzi wa huduma za matibabu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Dkt. David Mwenesano amesema Mfuko umejipanga kuwafikia wananchi wote kwa makundi yao pale walipo hivyo wana aina mbalimbali ya bima ya afya kwa wafanyakazi wa sekta rasmi na zisizo rasmi pamoja na mwananchi mmoja mmoja.

Amesema hivi sasa wanavyo vifurushi vya aina mbalimbali kulingana na hali ya wananchi na kila kifurushi mchangiaji anapata huduma zote zikiwemo matibabu na dawa”Mfano kuna makundi mbalimbali yameingia kama bodaboda,machinga hata wakulima na wavuvi lakini hata kama huna kikundi unaweza kuingia kupitia kifurushi cha najali,wekeza au timiza kwani viwango vya michango ni nafuu sana”.

Wakati huo huo Mkurugenzi wa idara ya tiba kutoka wizara ya afya Dkt. Grace Maghembe amesema kuwa suala ya watu kutokufanya mazoezi au kutojishughulisha mwili ni moja la tatizo la ongezeko la magonjwa yasiyoambukiza

Amewata wananchi wabadilishe mtindo wa maisha kwa kutokula vyakula vya wanga kwa kula kiasi wanachoweza kukitumia kwani ni kisibabishi cha mafuta ambayo yanakwenda kwenye mishipa ya moyo na kusababisha matatizo ya moyo na shinikizo la damu”turudi kwenye kula vyakula vyetu vya asili ikiwemo matunda na mboga mboga

Hata hivyo ameshauri wananchi kujenga tabia ya kwenda kupima afya zao walau mara mbili kwa mwaka kwani wagonjwa wengi wanaenda kwenye vituo vya kutolea huduma pale ugonjwa unapokuwa hatua nyingine ambayo inakua ngumu kutibika


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments