KATENGESYA AFUNGA MAFUNZO YA JINSIA NA MIPANGO YA BAJETI KWA WANAJAMII NA MAAFISA WATENDAJI MSALALA

Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Msalala mkoani Shinyanga Neema Katengesya akizungumza wakati akifunga mafunzo ya siku 6 ya Jinsia na Bajeti kwa mtazamo wa kijinsia kwa Wanajamii na Watendaji wa vijiji na kata za Shilela na Lunguya.

Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Msalala mkoani Shinyanga Neema amefunga mafunzo ya siku 6 ya Jinsia na Bajeti kwa mtazamo wa kijinsia kwa Wanajamii na Watendaji wa vijiji na kata za Shilela na Lunguya yaliyoandaliwa na Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) kwa ufadhili wa UNFPA na KOICA. 

Mafunzo hayo yaliyoanza siku ya Jumatatu Novemba 9,2020 na kumalizika leo Jumamosi Novemba 14,2020 katika ukumbi wa Mabingwa kata ya Bugarama Bugarama katika halmashauri ya Msalala yamekutanisha washiriki 60 wakiwemo wanajamii na viongozi wa ngazi ya vijiji, kata na halmashauri hiyo. 

Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo,Neema Katengesya ambaye ni Afisa Maendeleo ya Jamii Halmashauri ya wilaya ya Msalala ameushukuru Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) kwa kuandaa mafunzo hayo kwa ufadhili wa UNFPA na KOICA akieleza kuwa mafunzo hayo yatachochea mabadiliko ya kifikra katika jamii ili kuleta usawa wa kijinsia na kutokomeza vitendo vya ukatili. 

“Kwa niaba ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Msalala Kwa namna ya pekee sana niwashukuru TGNP, UNFPA na KOICA kwa kuwezesha kutolewa kwa mafunzo haya ambayo kimsingi yalitakiwa kutolewa na halmashauri,hivyo waturahisishia kazi”,alisema. 

“Miongoni mwa washiriki wa mafunzo haya yaliyoongozwa na mada ya Bajeti kwa mrengo wa kijinsia na mtazamo wa fikra kijinsia ni Wajumbe wa Kamati za MTAKUWWA, Maafisa Watendaji wa Kata na vijiji, Waragbishi na maafisa wa halmashauri ya wilaya. Kila mmoja akatekeleze majukumu yake, na mbegu iliyopandwa ikatuzalie tukapate matokeo mazuri”,ameongeza Katengesya. 

Katika hatua nyingine ameitaka jamii kuachana na mila na desturi kandamizi zinazochochea vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake ikiwemo Ngoma ya Mapacha (Ukango) ambapo washiriki wake hutumia matusi yanayogusa wanawake hivyo kudhalilisha wanawake. 

“Natamani huu utamaduni wa Ngoma ya Mapacha ya Wakango ubadilike. Wakango waache kutumia matusi, waongee lugha nzuri, Ukango iwe sherehe ya kufurahia kuzaliwa kwa watoto mapacha , wapewe zawadi kwa kuipongeza familia kuongeza familia na isiwaone watoto kama ni laana na mwanamke aheshimiwe”,ameongeza Katengesya.

Aidha amewataka maafisa watendaji wa kata na vijiji kushughulikia matukio ya ukatili dhidi ya wanawake na watoto kwa kuchukua hatua moja kwa moja badala ya kumaliza kesi kienyeji, wasikwepe kesi za matukio ya ukatili wa kijinsia, wala wasisukumiane kesi hizo. 

“Mtu asifanyiwe ukatili ili maendeleo yapatikane, wanawake wamiliki ardhi, wasibakwe, wasinyanyaswe,watoto waende shule. Kila mmoja aone kila kitu kwa mtazamo wa kijinsia na wanawake na wanaume wote washiriki katika masuala ya maendeleo”,amesema. 

Kwa upande wake, Mwezeshaji katika mafunzo hayo, Mwanaharakati wa masuala ya Jinsia na Haki za Binadamu, Bi. Gemma Akilimali aliwataka washiriki wa mafunzo wasikilize na kutazama jamii kile inahitaji, kisha watoe maoni kwenye vikao na mikutano ya vijiji na kata kuhusu vipaumbele vyao na kupanga mipango kutokana na mahitaji yao. 

“Wananchi washirikishwe katika upangaji wa bajeti kwa mrengo wa kijinsia kuanzia ngazi ya vijiji na kata na halmashauri ambapo wananchi wataibua fursa na vikwazo na kuainisha vitu wanavyovitaka ili vipangiwe bajeti kisha wanarudishiwa ili wananchi waamue nini hakitakiwi kukatwa katika bajeti”,amesema Gemma. 

“Katika kupanga bajeti kwa mrengo wa kijinsia, wananchi waanishe vipaumbele vya maendeleo ambavyo pia vinagusa masuala ya jinsia. Kunatakiwa kuwe na usawa wa kijinsia lakini pia mahitaji ya ujinsi lazima yaangaliwe”,aliongeza Gemma. 

Kwa upande wao washiriki wa mafunzo hayo waliishukuru UNFPA na KOICA kupitia TGNP kwa kuwapatia mafunzo hayo ambayo yamewabadili kifkra na kimtazamo kuhusu masuala ya jinsia na upangaji Bajeti kuanzia ngazi ya familia, kijiji na kata na wajibu wa jamii kufuatilia masuala ya bajeti. 
Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Msalala mkoani Shinyanga Neema Katengesya akizungumza wakati akifunga mafunzo ya siku 6 ya Jinsia na Bajeti kwa mtazamo wa kijinsia kwa Wanajamii na Watendaji wa vijiji na kata za Shilela na Lunguya katika ukumbi wa Mabingwa kata ya Bugarama leo Jumamosi Novemba 14,2020. Picha na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Msalala mkoani Shinyanga Neema Katengesya akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo.
Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Msalala mkoani Shinyanga Neema Katengesya akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo.
Mwanaharakati wa masuala ya Jinsia na Haki za Binadamu, Bi. Gemma Akilimali akitoa mada kuhusu Mipango ya Bajeti kwa mrengo wa kijinsia.
Mwanaharakati wa masuala ya Jinsia na Haki za Binadamu, Bi. Gemma Akilimali akitoa mada kuhusu Mipango ya Bajeti kwa mrengo wa kijinsia.
Washiriki wa mafunzo hayo wakiwa ukumbini.
Washiriki wa mafunzo wakiwa ukumbini.
Mafunzo yanaendelea
Mafunzo yanaendelea
Washiriki wa mafunzo wakiwa ukumbini.

Picha zote na Kadama Malunde - Malunde 1 blog

Soma pia : 

GEMMA : WANAUME MSITISHWE NA KASI YA MABADILIKO YA WANAWAKE..."MSITUMIE MFUMO DUME KULIPA KISASI"


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments