Breaking : HALIMA MDEE NA WENZAKE WALIOAPISHWA UBUNGE DODOMA WAFUKUZWA CHADEMA USIKU HUU

Spika wa Bunge, Mheshimiwa Job Ndugai akiwa katika picha ya pamoja na Wabunge wa Viti Maalum CHADEMA baada ya kuapishwa kwenye Viwanja vya Bunge Jijini Dodoma hivi karibuni
**
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) nchini Tanzania, kimetangaza kuwafukuzwa uanachama wanachama Halima Mdee na wenzake 18 kwa tuhuma za usaliti. Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam.

Uamuzi huo umetangazwa leo saa 5:11 usiku Ijumaa tarehe 27 Novemba 2020 na Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe wakati akizungumza na waandishi wa habari akitoa maazimio ya kikao cha kamati kuu.

Kikao cha kamati kuu kimefanyika kuanzia asubuhi leo katika Hoteli ya Bahati Beach jijini Dar es Salaam huku wajumbe wawili wa kikao hicho, Tundu Lissu, makamu mwenyekiti wa Chadema-bara na Ezekiel Wenje wakishiriki kwa njia ya mtandao.

Mdee na wenzake 18, walikuwa wakituhumiwa kujipeleka bungeni na kuapishwa tarehe 24 Novemba 2020 na Spika Job Ndugai wakijua chama hicho hakijatea majina ya wabunge wa viti maalum.

Wabunge wengine waliofukuzwa ni wajumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, Ester Bulaya na Esther Matiko. Katibu Mkuu wa Bavicha, Nusrat Hanje. Katibu Mkuu Baraza la Wanawake Chadema (Bawacha), na Grace Tendega.


Mbowe amesema, “Huwezi kupendekezwa na chama cha siasa, huwezi kupendekezwa na mtu yoyote kwani Tanzania hatuna mgombea binafsi. Sasa huwezi kupendekezwa na mtu yoyote yule,” amesema Mbowe.

“Wabunge wetu hawa 19, mama zangu na dada zangu wameapishwa kiapo batili kwani Katiba inasema waapishwe mbele ya Bunge. Sasa kanuni zimebadilishwa ili kumruhusu Spika kumwapisha popote hata eneo la gereji.”

“Kamati kuu imewavua nyadhifa zao zote ndani ya chama na kuanzia sasa wasijihusishe kwa namna yoyote na masuala ya chama. Wako waliokuwa viongozi Bawacha na wengine Bavicha. Kamati tendaji za mabaraza hayo zikutane kujaza nafasi hizo.”

“Kiapo kilicholiwa Dodoma na mchakato mzima wa kuwapata, umegubikwa na uongo, kughushi na ulikuwa batili. Tumeagiza kurugenzi yetu kupinga huo uteuzi wa wabunge 19 na tutaupinga kwani chama hakijapelela majina,” amesema Mbowe

 Chanzo MwanahalisiOnline

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments