Ofisi Ya Ardhi Tabora Yatatua Mgogoro Kati Ya Bibi Na Kanisa La EAGT Uliodumu Zaidi Ya Miaka 20


 Na Munir Shemweta, WANMM TABORA
Ofisi ya Ardhi Mkoa wa Tanga imetatua mgogoro wa ardhi uliodumu kwa zaidi ya miaka 20 kati ya Kanisa la EAGT na bibi Tamasha Mhanuka kwenye eneo la mtaa wa Bakari Manispaa ya Tabora mkoani Tabora na kumkabidhi Hati.

Bibi Tamasha kwa muda mrefu amekuwa na mgogoro na Kanisa la EAGT lililotaka   kulichukua eneo hilo na maeneo ya wakazi wengine watano kwa ajili ya kuendesha shughuli za kanisa. Hata hivyo, wamiliki wa maeneo hayo walishindwa kukubaliana na Kanisa kuhusiana na fidia ya kuwaondoa.

Timu ya Ofisi ya Ardhi mkoa wa Tabora ikioongozwa na Kamishna Msaidizi wa Ardhi Jabir Singano juzi ilikwenda eneo la Bi Tamasha lililopo mtaa wa Bakari njia kuu ya kuelekea Kigoma katika Manispaa ya Tabora na kumkabidhi Hati ya Ardhi sambamba na kumuonesha mipaka ya eneo lake ili aweze kufanya maendelezo aliyoshindwa kufanya kutokana na mgogoro huo.

Mkuu wa idara ya ardhi Manispaa ya Tabora Deo Damian Msilu alisema, chimbuko la mgogoro huo baina ya Bi. Tamasha na Kanisa la EAGT lilisababishwa na eneo hilo kuwa katika mpango wa matumizi ya umma yaani taasisi za dini na kupewa kanisa la EAGT.

Kwa mujibu wa Msilu, kilichotakiwa kufanyika ni uthamini wa kumlipa bibi Tamasha pamoja na wakazi wengine watano aliyekataa kuchukua fidia jambo lililosababisha ofisi ya ardhi mkoa wa Tabora kubadilisha mpango wa matumizi ya eneo hilo na kuwa makazi.

Kwa upande wake kamishna Msaidizi wa Ardhi mkoa wa Tabora Jabir Singano alisema, ofisi yake imekuwa ikishirika kutatua migogoro ya ardhi katika mkoa huo na moja ya mgogoro uliofanyiwa kazi ni wa bibi Tamasha na kanisa la EAGT.

Singano alisema, suala la mgogoro huo awali lilishughulikiwa na halmashauri ya Manispaa ya Tabora lakini halikupata ufumbuzi jambo lililoifanya ofisi yake mara baada ya kuanza kazi kuamua kulifanyia kazi hasa ikizingatiwa moja ya kazi ya ofisi hiyo ni kuhakikisha wanyonge wanabaki katika miji.

‘’Eneo la huyu bibi zuri kama mnavyoona liko katika barabara kuu ya kuelekea Kigoma na ni barabara ya lami na stendi iko umbali wa takriban kilometa moja, tuliliita kanisa na kuzungumza nalo ingawa kuna baadhi ya vipande lilipa fidia lakini kwa kuwa eneo hili lilikuwa ni utoaji binafsi ilibidi waachwe.

Kamishna Msaidizi wa Ardhi mkoa wa Tabora aliongeza kwa kusema kuwa, baada ya kufikia muafaka na pande zote mbili waliamua kupima viwanja vitano na kuwaandalia Ankara ya malipo wamiliki wake ili watakapokamilisha wapatiwe hati na kumshukuru Mungu kwa kufanikisha kutatua mgogoro huo alioueleza kuwa ulikuwa ukimfanya Bi. Tamasha kushindwa kufanya maendelezo ya eneo kutokana na kutojua mipaka.

Singano alisema, kwa wananchi wote wenye migogoro ya aina hiyo waifikishe ofisi ya ardhi mkoa wa Tabora ili kupatiwa ufumbuzi na kusisitiza kuwa ofisi hiyo iko kwa ajili ya kutetea haki  ya kila mtu na aliye na haki atapata haki yake na aliyepora haki ya mtu atairudisha.

Naye Bi. Tamasha Mhanuka aliishukuru ofisi ya Adhi mkoa wa Tabora hasa Kamisha Msaidizi wa Ardhi Jabir Singano pamoja na Afisa Mipango Miji Faraji Shemgha kwa kusaidia kutatua mgogoro huo na kufanikisha kupatiwa hati ya eneo lake.

Aidha, Bi. Tamasha aliiomba serikali na wananchi wenye uwezo kumsaidia kufanikisha ujenzi wa nyumba yake aliyoieleza kuwa haiku katika hali nzuri.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments