MANYONI YAGEUKA KIVUTIO MASHAMBA YA KOROSHO



Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Tixon Nzunda  akizungumza jana kwenye Kitongoji cha Masigati wilaya ya Manyoni, eneo ambalo kuna shamba kubwa la mikorosho lenye takribani ekari elfu.


Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Tixon Nzunda  akizungumza na wakulima aliposhiriki sehemu ya programu maalumu ya mafunzo kwa vitendo inayotolewa na serikali kwa wakulima na maafisa ugani kupitia TARI Naliendele kwa kushirikiana na Bodi ya Korosho.
Mkurugenzi wa Maendeleo ya Mazao kutoka Wizara ya Kilimo, Nyasebwa Chimagu akizungumza kwenye mafunzo hayo.
 Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Manyoni, Charles Fussi akizungumza na wanahabari muda mfupi baada ya kufungua mafunzo hayo.
Baadhi ya Watafiti kutoka TARI Naliendele wakimsikiliza mmoja wa wadau wa zao la Korosho
Wakulima na Maafisa Ugani wakiwa kwenye mafunzo kwa vitendo, hatua ya upogoleaji mkorosho
 Mwakilishi wa Kikundi cha Food and Drinks (FND) kutoka Dar es Salaam, Mussa Tambo Compound akizungumza baada ya kushiriki mafunzo hayo kwa vitendo kwenye shamba la Masigati.
Mwonekano wa mkorosho ambao umeanza kutoa maua kwenye moja ya shamba la masigati Manyoni.
Baadhi ya alama muhimu zilizowekwa na viongozi wakati wa uanzishaji wa mashamba hayo.
Mtafiti Mwandamizi kutoka Kitengo cha magonjwa ya mikorosho na visumbufu vya wadudu kutoka TARI Naliendele, Dkt Wilson Nene akifundisha wakulima namna ya utambuzi wa magonjwa hususani ugonjwa wa Ubwiriunga na wadudu vamizi wa mikorosho.
Mafunzo ya namna ya kupogolea mkorosho kwa vitendo.
Mafunzo ya upimaji yakiendelea.
Meneja wa Bodi ya Korosho Kanda ya Kati na Magharibi, Ray Mtangi akishiriki programu hiyo kikamilifu.
Mratibu wa zao la Korosho nchini, Dkt Geradina Mzena akiwa na wageni mbalimbali waliotembelea shambani hapo ili kujifunza Kilimo Bora cha zao hilo.


 Na Godwin Myovela na Dotto Mwaibale, Singida


MAMIA ya wakulima kutoka maeneo mbalimbali nchini
wameendelea kujitokeza kwenye mashamba makubwa ya Korosho yaliyopo eneo la Masigati, Wilaya ya Manyoni, mkoani hapa ili kujifunza teknolojia za uzalishaji wa zao hilo kwa vitendo.

 Mashamba hayo ambayo mikorosho yake imeoteshwa kwa umahiri na ustadi mkubwa, kwa kuzingatia teknolojia za kisasa, kwa sasa yamegeuka kuwa kivutio na hamasa kubwa kwa kila
anayetembelea eneo hilo na kujikuta akivutiwa kuanza kulima ‘dhahabu hiyo ya kijani.’

Katibu Mkuu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Tixon Nzunda ni
miongoni mwa wakulima, maafisa ugani na watanzania wengine waliopata fursa ya kushiriki sehemu ya mafunzo kwa vitendo ya Kilimo Bora cha zao la Korosho kwenye eneo hilo yanayoendelea kutolewa na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo (TARI) Naliendele kwa kushirikiana na Bodi ya Korosho.

Wengine waliofika kufuatilia mafunzo hayo kwa nyakati
tofauti ni Mkurugenzi wa Maendeleo ya Mazao, Nyasebwa Chimagu, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Manyoni Charles Fussi, na kikundi cha wakulima na Wajasiriamali kwa njia ya mtandao kutoka jiji la Dar es Salaam na Dodoma
kinachojulikana kama Food and Drinks (FND)

Akizungumza kwenye eneo hilo la mafunzo, Nzunda alisema mafunzo hayo yamekuja kwa wakati mwafaka, huku akiomba Wizara ya Kilimo kupeleka wataalamu wake wa kudumu kwenye maeneo ya mashamba hayo ili kuwajengea uwezo wakulima.

Aidha, alipongeza Wizara ya Kilimo kupitia TARI Naliendele kwa
kuanza kuitikia wito wa kujenga uwezo wa huduma za kiugani kwa wakulima wadogo, huku akisisitiza hatua hiyo ni mwanzo mzuri wa kusonga mbele kwenye kilimo cha korosho kutoka kile cha kienyeji kwenda kwenye kilimo cha kibiashara.

Nzunda alishauri mathalani eneo hilo la Masigati kuimarishwa
kwa mfumo mahususi utakaohakikisha wakulima wote wa eneo hilo na wanapatiwa mafunzo ya pamoja kuanzia kwenye kuandaa mashamba, upimaji, ushimbaji mashimo, upandaji, palizi hadi upogoleaji lakini pia wanapata fursa ya huduma za ugani kwa pamoja.

Alisema binafsi anaamini miaka michache ijayo mradi huo
mahiri wa masigati unakwenda kuwa kitovu cha mafunzo kwa nchi nyingine za Afrika Mashariki, Afrika ya Kati, Kusini mwa Jangwa la Sahara na dunia kwa ujumla.

 “Wataalamu tokeni wizarani njooni mkae huku na wakulima…saidieni tunataka Manyoni hii iwe ‘Modal’ kwenye zao la korosho, mwamko ni mkubwa, tuendelee kufanya ‘Outrich Programs’
za kutosha ili kujenga uwezo kwa wakulima hawa na tukifanya hivi kilimo cha korosho kwenye kanda hii ya kati kitakuwa cha mfano,” alisema Nzunda.

 Kwa upande wake, Mkulima kutoka Manyoni, Joel Bulari alipongeza serikali kuja na mafunzo hayo ambayo sasa yamempa mwanga wa kulifahamu kwa undani zao hilo hatua kwa hatua
kuanzia maandalizi ya shamba, upimaji wa shamba jipya, na namna ya kupanda mbegu bora na hatua za upogoleaji.

Mkulima mwingine, Rehema Mnyapara kutoka Kata ya Mhalala,
Manyoni anasema nimejifunza na kuona fursa nyingi sana kwenye kilimo cha korosho. Kilichonivutia zaidi ni kuwa zao hili halihitaji maji mengi na pia soko lake ni la uhakika.

Mwakilishi kutoka kikundi cha (FND) Jacqueline Kitundu
alisema wamevutiwa sana na mafunzo hayo na hatua itakayofuata ni yeye na wenzake kuja kununua mashamba mapya na kuanza kilimo cha zao la korosho.  

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527