YANGA SC WAICHAPA MTIBWA SUGAR 1 - 0

Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
VIGOGO, Yanga SC wameendeleza staili yao ya ushindi mwembamba katika Ligi Kuu ya Tanzania Bara baada ya leo pia kuichapa Mtibwa Sugar 1-0 Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro.

Pongezi kwa mfungaji wa bao hilo pekee, beki Mghana, Lamine Moro aliyeunganisha kwa mguu wa kulia kona ya chini chini ya kiungo Muangola, Carlos Carlinhos dakika ya 61.

Na kwa ushindi huo, Yanga SC inafikisha pointi 10, sawa na mabingwa watetezi, Simba SC ambao wanaendelea kukaa nafasi ya pili kwa faida ya mabao mengi waliovuna baada ya mechi nne za awali.

Azam FC inaendelea kuongoza baada ya kufanikiwa kushinda mechi zake zote nne za awali, wakiwa na pointi 12. 

Mechi nyingine za Ligi Kuu leo, Ruvu Shooting imelazimishwa sare ya bila kufungana na Biashara United Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.

Mwadui FC imeibuka na ushindi wa 2-0 dhidi ya Ihefu, mabao ya Fred Felx dakika ya sita na Wallace Kiango dakika ya 37 Uwanja wa Mwadui Complex, Kishapu mkoani Shinyanga.

Raundi ya Nne ya Ligi Kuu itakamilishwa kesho kwa mchezo mmoja tu, Coastal Union wakiwa wenyeji wa JKT Tanzania kuanzia Saa 10:00 jioni Uwanja wa Mkwakwani Jijini Tanga.

Kikosi cha Mtibwa Sugar kilikuwa; Abdultwalib Mshery, Hassan Kessy, Issa Rashid ‘Baba Ubaya’, Geoffrey Kiggi, Dickson Job, Baraka Majogoro/ Awadh Juma dk75, Joseph Mkele, Boban Zirintusa/ Juma Nyangi dk35, Ibrahim Hilika, Salum Kihimbwa/Riphat Msuya dk65 na Haroun Chanongo. 

Yangs SC; Metacha Mnata, Kibwana Shomari, Yassin Mustapha, Lamine Moro, Bakari Mwamnyeto, Feisal Salum, Zawadi Mauya, Mukoko Tonombe, Michael Sarpong/Ditram Nchimbi dk85, Carlos Carlinhos/ Yacouba Sogne dk70 na Tuisila Kisinda/Haruna Niyonzima dk89.

 Chanzo - Binzubeiry blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527