RAIS WA MALI AJIUZULU BAADA YA KUKAMATWA NA WANAJESHI WAASI


Rais wa Mali, Ibrahim Boubacar Keïta amejiuzulu muda mfupi baada ya kuwekwa kizuizini na Jeshi la nchi hiyo.

Akilihutubia taifa kwa njia ya televisheni, Bwana Keïta amesema anaivunja serikali na bunge.

''Sitaki damu imwagike ili mimi kuendelea kubaki madarakani,'' aliongeza.

Hatua hii imekuja saa kadhaa baada ya kiongozi huyo wa juu na Waziri Mkuu Boubou Cissé kupelekwa kwenye kambi ya jeshi karibu na mji mkuu Bamako, hatua iliyosababisha mataifa ya Afrika Magharibi na Ufaransa kulaani kitendo hicho.

''Ikiwa leo, sehemu ya vikosi vilivyo na silaha wanataka hili liishe kwa kuingilia kati, nina cha kufanya?'' alisema Keïta.

Rais huyo pamoja na waziri mkuu wake walikamwatwa na jeshi baada ya maandamano yaliyodumu kwa miezi kadhaa kumtaka bwana Keita kung'atuka madarakani.

Keita ambaye alikua katika muhula wake wa pili wa uongozi alikua akituhumiwa kusababisha mdororo wa kiuchumi nchini humo pamoja na kushindwa kuyazuia makundi ya wapiganaji wa kiislamu ambayo yameharibu amani ya nchi hiyo.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527