IGP SIRRO AWAONYA WANASIASA WALIOANZA KUONYESHA SHARI KUPITIA MATAMSHI YAO KUELEKEA UCHAGUZI MKUU, OKTOBA 2020


Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP), Simon Sirro, amewaonya wanasiasa walioanza kuonyesha shari kupitia matamshi yao kuelekea uchaguzi mkuu, Oktoba 2020 na kuwataka kutolilaumu jeshi lake litakapochukua hatua dhidi yao.



“Wao wanachozungumzia si uchaguzi wa amani na utulivu, sera yao ni ushari, sasa ninavyoona mazingira ya baadhi ya viongozi, sitaki kuwataja, Watanzania tunaona, sasa ukiona viongozi wanaanza na ushari, kesho wasilaumu vyombo vya dola,” amesema IGP Sirro wakati akihojiwa kwenye kipindi cha Dakika 45 cha ITV wiki hii

“Nimeona viongozi wa siasa wanazungumza mambo makali sana. Ninawaheshimu viongozi wote wa siasa katika ngazi zote lakini lazima sheria na kanuni zilizopo ziheshimiwe.

"Ukiangalia baadhi ya viongozi wanavyozungumza, unaona kuna ushari. Ushari wanauonesha wanaupeleka kwa washabiki wao wawe na ushari huo huo.” -Alisema IGP Sirro

Alisema, Watanzania wengi hawana mazoea na shida na hawataki shida zinazotokana na uchaguzi ambapo amesisitiza kwamba kuna maisha baada ya uchaguzi.

“Watanzania wengi hawataki shida, lakini uchaguzi utapita na tutaendelea kuishi na sisi tuna watoto, tuna wajukuu tuna nani. Tunataka nchi yetu iendelee kuwa na amani na utulivu.

“Hii habari ya maneno ya kusema mimi nimeishasema nimemaliza, hakuna aliyeko juu ya sharia, Watanzania wengi wanapenda amani,” alisema.

Alisema, kwa kuwa ana dhamana ya ulinzi na usalama, wanaojiandaa kwa ushari wajue watawakabili kwa mujibu wa sheria .




Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527