AHMED SALUM ASHINDA KURA ZA MAONI JIMBO LA SOLWA... AMZIDI AZZA HILAL KURA 73


Ahmed Salum akizungumza wakati wa kujinadi kabla ya zoezi la upigaji kura
Azzah Hilal akizungumza mapema kabla ya zoezi la upigaji kura

Na Damian Masyenene -Shinyanga Press Club Blog
JITIHADA za Kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ahmed Salum kutetea kiti cha Ubunge wa Jimbo la Solwa mkoani Shinyanga zinazidi kuzaa matunda baada ya hii leo kushinda kura za maoni jimboni humo

Ahmed Salum ameliongoza Jimbo la Solwa kwa muda wa miaka 15 (2005-2020).

Zoezi la upigaji kura za maoni kwa watia nia wa ubunge jimbo la Solwa lilianza leo Julai 20, 2020 katika Uwanja wa CCM Kambarage, mjini Shinyanga majira ya saa 8 mchana (watia nia kujieleza) na saa 12 jioni zoezi la kuhesabu kura likaanza hadi saa 2 usiku.

Ambapo jumla ya watia 54 waliomba ridhaa ya CCM kuwateua ili wagombee ubunge jimboni humo, huku ushindani ukiwa kwa aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Shinyanga, Azzah Hilal Hamad (CCM) na aliyekuwa Mbunge wa Jimbo hilo, Ahmed Salum.

Kwa Mujibu wa Msimamizi Mkuu wa zoezi hilo, Peter Gawiza ambaye ni Mjumbe Kamati ya Siasa ya Wilaya ya Shinyanga Vijijini na Mwenyekiti wa Wazazi CCM wilayani humo, wajumbe waliotakiwa kuhudhuria uchaguzi huo ni 843, waliohudhuria ni 834, waliopiga kura ni 823, kura zilizoharibika ni 0 na kura halali ni 823.

Gawiza alimtangaza Ahmed Salum mshindi wa kura hizo baada ya kupata kura 377 dhidi ya 304 za mpinzani wake wa karibu, Azzah Hilal, huku Jeremiah Jilili akiibuka mshindi wa tatu kwa kura 35, Sosthenes Katwale kura 21, SPA Mussa Singu (20) na Amos Mshandete kura 12.

Kwa mujibu wa Gawiza, watia nia 25 hawakupata kura hata moja, 10 walipata kura moja kila mmoja, sita wakapata kura mbili kila mmoja, wawili wakaambulia kura tatu tatu, wawili wakapata nne kila mmoja na wawili wengine wakaambulia kura tano kila mmoja.

Akitoa neno kwa wagombea, Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Jasinta Mboneko amewapongeza watia nia wote waliogombea, huku akisistiza kwamba kinachoshinda ni chama (CCM) na siyo mtu, hivyo amewataka wote kuhakikisha chama hicho kinaibuka na ushindi kwenye uchaguzi mkuu ujao na pia wagombea kufanya kampeni za kistaarabu.

Chanzo - Shinyanga Press Club blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527