TAKUKURU DODOMA YAMREJESHEA MSTAAFU MILIONI 10 ALIZODHURUMIWA NA TAASISI YA FEDHA YA SWAHILI TRUST MICROFINANCE

Na.Faustine Gimu Galafoni,Dodoma.

Taasisi ya kuzuia  na kupambana na Rushwa [TAKUKURU]Mkoa wa Dodoma imefanikiwa kumrejeshea kiasi cha Tsh.milioni kumi  Bi.Frida  Nahamani mwenye umri wa miaka 62 mkazi wa Michese jijini Dodoma alizodhurumiwa na Bw.Maswe  Wambura Mgaya ambaye ni mmiliki wa Taasisi ya SWAHILI TRUST MICROFINANCE  ya jijini  Dodoma inayofanya biashara ya ukopeshaji wa fedha.


Akizungumza na Waandishi wa Habari leo Juni 26,2020  ofisini kwake,mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Dodoma Bw.Sosthenes Kibwengo amesema uchunguzi ulianzishwa mara baada ya kupokea malalamiko ya Bi.Nahamani muuguzi mstaafu ambapo uchunguzi huo ulionesha kuwa kati ya Julai na Disemba ,2018 alikopa kiasi cha shilingi milioni  kumi na tano[15,000,000/=]na akakabidhi kadi yake ya  benki kwa taasisi hiyo ili warejeshe fedha zao mara mafao yake ya kustaafu yakitoka .

Bw.Kibwengo amesema ,Mstaafu aliporejeshewa kadi yake  tarehe 31/1/2019 alikuta akaunti yake haina fedha yoyote ilihali alipokea mafao yake zaidi ya Tsh.Milioni arobaini na sita[46].

“Baada ya uchunguzi tumejiridhisha ya kwamba  SWAHILI TRUST MICROFINANCE ilizidisha kiasi cha Tsh.milioni kumi kwenye makato yao na ndio wamezirejesha baada ya TAKUKURU mkoa wa Dodoma kuingilia kati na kuwataka kufanya hivyo”amesema Kibwengo.

Katika hatua nyingine, Bw.Kibwengo amesema  kuwa TAKUKURU mkoa wa Dodoma leo Juni,26,2020 inawakabidhi viongozi  wa vyama vya akiba na mikopo [SACCOS]vya MWASHITA na DUWASA  jumla ya Tsh.milioni 74.2 zilizokuwa mikononi mwa wanachama 32 waliokuwa na madeni kwa muda mrefu.

Aidha,Bw.Kibwengo amebainisha kuwa,TAKUKURU mkoani Dodoma inawasilisha kiasi cha Tsh.milioni tisa na laki tatu na elfu kumi kwa uongozi wa mkoa wa Dodoma za vitambulisho vya wajasiriamali zilizotolewa kutoka kwa watumishi 37 wa halmashauri ya Wilaya ya Chamwino pamoja na kukusanya vitambulisho 270 vyenye thamani ya Tsh.milioni tano na laki
nne[5,400,000/=]
__________________________


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527