AJALI YA DALADALA KUGONGA TRENI NA KUSABABISHA KIFO NA MAJERUHI


Mnamo Tarehe 12.6.2020 majira ya saa 17.20hrs huko maeneo ya Mwakanga kwenye makutano ya njia ya reli na barabara itokayo Chanika kwenda Pugu wilaya ya Ilala Mkoa wa Dar es Salaam, treni ya abiria iliyokuwa ikitokea Stesheni ya TAZARA Dar es Salaam kuelekea Mbeya ikiendeshwa na Judith Lupenzi na Rita Mduma iligongwa na Gari aina ya daladala no T503 CMZ aina ya EICHER lililokuwa likitokea Chanika kwenda Buguruni na kusababisha kifo Cha abiria mmoja mwanaume aliyejulikana kwa jina la Salehe Iddi miaka 40 Msambaa na mkazi wa Kariakoo na majeruhi 20 Kati ya majeruhi hao watano ni watoto.

Katika uchunguzi wa awali wa Polisi uliofanyika baada ya kutokea ajali hiyo imebainisha kwamba chanzo cha ajali hiyo ni uzembe wa dereva wa daladala kushindwa kufuata Sheria za usalama barabarani jambo ambalo linagharimu maisha ya watu na mali.

Jeshi la Polisi kikosi cha TAZARA linaendelea kumtafuta dereva wa Gari hilo ambaye alikimbia baada kutokea ajali hiyo ili sheria ichukue mkondo wake. Majeruhi walikimbizwa hospitali ya Pugu Kajiungeni kwa matibabu na hali zao kwa mujibu wa taarifa za daktari wanaendelea vizuri.

Mwili wa marehemu ulipelekwa hospitali ya Mwananyamala kwa uchunguzi zaidi.

Niendelee kutoa wito kwa wananchi ikiwemo vyombo vyote vya moto kama magari kuheshimu sheria za usalama barabarani kwani katika vivuko vya reli zipo alama ambazo kama dereva ama mtembea kwa miguu anatakiwa kuzifuata kabla ya kuvuka.

Aidha, katika maeneo yote yanayopitiwa na miundombinu ya reli ya TAZARA wananchi waendelee kuthamini na kulinda miundombinu hiyo kwani ni faida kwao kama chanzo cha mapato na Uchumi wa nchi kwa ujumla.

IMEANDALIWA NA:
ACP Advera John Bulimba,
KAMANDA WA KIKOSI CHA POLISI TAZARA


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527