NDEGE YATUA MWANZA KUBEBA MINOFU YA SAMAKI…MHANDISI STELLA MANYANYA ATANGAZA SOKO LA SAMAKI WA KANDA YA ZIWA

Na Eliud Rwechungura – Wizara ya Viwanda na Biashara
Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Mhandisi Stella M. Manyanya ametangaza fursa za soko la samaki kanda ya ziwa.


Mhe. Manyanya ameyasema hayo 21 mei 2020 katika shughuli ya mapokezi ya ndege ya Ethiopia  Airlines iliyoanza safari zake kuja Tanzania katika mkoa wa Mwanza  kuchukua minofu ya samaki ambao inauzwa katika nchi mbalimbali.

Mhe. Manyanya amesema kuwa "Mpaka kufikia mwezi machi 2020 samaki Tani 392,933 wamevunwa nchini na mauzo yameongezeka kulingana na miaka miwili iliyopita ambapo mauzo yalikuwa Bilioni 379 na kufikia bilioni 691.88 kwa mwaka 2018/2019. Tani 32,388.88 zenye thamani ya Bilioni 436.97 ziliuzwa nje ya nchi na mapato kwa Serikali yalikuwa bilioni 19.1"

Mhe. Manyanya baada ya kujionea ndege ya Ethiopia Airline ikipakia samaki ametumia fursa hiyo kuwatangazia na kuwadhihirishia wawekezaji wote nchini kuwa kuna soko la samaki la uhakika kwasababu kwa sasa samaki zinafatwa moja kwa moja mkoa wa mwanza na kupelekwa katika maeneo mbalimbali duniani kote.

“Tanzania tumejariwa, tunao samaki wazuri na wakutosha na sio ziwa victoria tu tuna majiziwa mengine makubwa na bahari ya hindi, kwa hiyo naomba niwadhihirishie wawekezaji wote kuwa sasa tuna soko la uhakika la samaki kwahiyo jitokezeni kuwekeza kwasababu minofu yetu ya samaki inafatwa moja kwa moja na ndege hadi mkoa wa Mwanza”

Aidha amesisitiza kuwa "Ndege ya Ethiopia iliyoanza kuja  21 mei 2020 imepakia kilogram 17,262 zenye thamani ya Tsh. 191,874,837.78 na mrabaha uliolipwa ni Tsh. 9,541,301.21 na samaki hizo zitauzwa katika nchi za Belgum, Holand, Germany, France, Portugal na Australia na kwa upande wa mabondo (fish maws) soko kubwa ni china"

Nae Naibu wa Ujenzi, Uchukuzi na Masiliano Mhandisi, Atashasta J Nditiye amesema kuwa safari za ndege ya Ethiopia kuja kuchukua samaki hapa Mwanza ni fursa kubwa kwa wana Mwanza na Kanda ya ziwa kwa ujumla maana kabla ya hapo ilikuwa inakuja ndege ya Rwanda Air ambayo ilikuwa inakuja mara moja kwa wiki kila jumanne Lakini Ethiopia Airlines imeanza safari leo na bado ratiba yake haijajulikana.

Kwa upande wa Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. John Mongella amesema kuwa ni viwanda vitatu vilinavyosafirisha samaki  ambavyo ni (i) Kiwanda cha Victoria Perch limited ambao wanasafirisha Tani 5.4 (5,400kg) zenye thamani ya USD 21,600 (ii) Kiwanda cha Nile Perch Limited ambao wanasafirisha  Tani 8.9 (8990kg) zenye thamani ya USD 35,900  (iii) Kiwanda cha Omega Fish limited kinachosafirisha Tani 5 (5,000kg) zenye thamani ya USD 22,320.

Aidha, Mongella amesisitiza kuwa Uzalishaji wa kanda ya ziwa kwa wastani kila wiki katika kipindi cha mavuno ni wastani wa Tani 1100 na kipindi mavuno haba ni tani 220.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527