KALIUA YATOA MKOPO WA MILIONI 345 KWA VIKUNDI 57 KATIKA KUSHEREKEA SIKU YA WANAWAKE DUNIANI

NA TIGANYA VINCENT
HALMASHAURI ya Wilaya ya Kaliua imekabidhi mkopo wa shilingi milioni 345 kwa vikundi 57 ikiwa ni sehemu ya asilimia 10 ya mapato yake ya ndani katika mwaka wa fedha unaoendelea.


Taarifa hiyo imetolewa jana na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo Dkt. John Pima wakati wa maadhimisho ya siku ya wanawake duniani ambayo kimkoa yalifanyika jana Wilayani humo.

Alisema kati ya fedha hizo vikundi 28 vya wanawake vimepokea milioni 184, vikundi 19 vya vijana vimekopeshwa 133.5 na vikundi 10 vya walemavu vimekpeshwa milioni 27.

Alisema fedha hizo ni sehemu ya utekelezaji ilani yaChama cha Mapinduzi iliyoagiza kutenga asilimia 10 kutokana na mapato ya ndani kwa ajili ya mikopo kwa vikundi hivyo.

Dkt Pima alisema tangu nwaka 2015 hadi desemba 2019 , Kaliua ilikuwa imeshatoa jumla ya mikopo ya shilingi milioni 839.7 kwa vikundi 209.

Aidha Mkurugenzi huyo alisema hadi hivi jumla ya shilingi milioni 591.9 bado haijarejeshwa kitendo ambacho kimewafanya waandikie notisi ya 90 ili warejeshe.

Dkt. Pima alisema baada ya hapo wadaiwa sugu wote watachukuliwa hatua za kisheria.

Akikabidhi hundi kwa vikundi , Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri amevitaka vikundi ambavyo bado havijaresha mikopo waliopatiwa kurejesha ili iweze kuwasadia wengine.

Aliipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua na kuzitaka Halmashauri nyingine za Mkoa wa Tabora kuhakikisha wanatenga asilimia 10 za mapato yake ya ndani kwa ajili ya kupeleka katika vikundi kama ilivyoelekezwa.

Mwanri alisema kuwa ni vema Halmashauri zikahakikisha zinatoa fedha ambazo zitavisaidia vikundi kupata matokeo mazuri na kuwapatia maendeleo.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post