WAZIRI WA KILIMO: MAZAO YOTE YA KIMKAKATI YANASIMAMIWA NA BODI ZA MAZAO SIO USHIRIKA

Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo-Dodoma

Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga (Mb) ameliarifu Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa mazao yote ya kimkakati yanasimamiwa na Bodi za Mazao husika sio vyama vya Ushirika.

Mhe Hasunga ameyasema hayo leo tarehe 3 Februari 2020 wakati akijibu maswali Bungeni ambapo amesisitiza kuwa vyama vya Ushirika vina jukumu la kukusanya mazao na kuyapeleka sokoni kwa ajili ya kuuza kwa niaba ya wanachama sio kusimamia uzalishaji.

Amesema kuwa jambo hilo litaendelea vivyo hivyo na kuwekewa mkakati wa kuimarishwa zaidi ili kuwasaidia wakulima kunufaika na kipato kinachotokana na tija katika uzalishaji wa mazao nchini.

“Tunataka mazao yote, pembejeo zote kuanzia (mbegu, mbolea, viuadudu) hivi vyote vitakuwa vinasambazwa na sekta binafsi katika maeneo yote sio serikali” Alikaririwa Mhe Hasunga

Kadhalika, amewataka wafanyabiashara kuchangamkia fursa hiyo ya kuuza viuatilifu kwani serikali inaendelea kuruhusu sekta binafsi kupeleka viuadudu kwenye mazao mbalimbali kama vile Korosho, Pamba, Kahawa na mazao mengine yote.

Ameongeza kuwa jukumu la serikali itakuwa ni kusimamia na kuratibu maendeleo ya mazao husika na namna ya kutafuta masoko lakini sio kusambaza pembejeo.

Mhe Hasunga amesema kuwa hiyo ni fursa kwa watanzania wote wanaotaka kufanya biashara hiyo kujitokeza kwa wingi.

Waziri Hasunga amesema kuwa baadhi ya viongozi wa vyama vya Ushirika waliingia kwenye biashara ya Tumbaku na kuuza zao hilo bila kufuata utaratibu hivyo kuathiri bei ambayo ingetokana na soko.

Amesema Kutokana na changamoto hiyo Wizara ya kilimo ilikabidhi taarifa ya uchunguzi kwenye uongozi wa Taasisi ya kuzuia na kupambana na Rushwa (TAKUKURU) ili kuwachukulia hatua viongozi wote waliokiuka maadili ya uongozi na wale ambao hawakusimamia mazao ipasavyo hivyo kusababisha hasara kwa wananchi na vyama vya Ushirika.

Zoezi hilo linaendelea nchi nzima kwani viongozi husika wanakamatwa na kuchukuliwa hatua ikiwemo kurejesha fedha walizopora.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post