WAZIRI LUGOLA AWAONDOA MADARAKANI MAAFISA WA NIDA MKOA WA RUVUMA

Na Mwandishi Wetu, MOHA, Songea.

WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi Kangi Lugola  amemuondoa madarakani Afisa wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) Mkoa wa Ruvuma, Seif Mgonja kwa kosa la kutogawa kwa wananchi Namba za Utambulisho wa Taifa (NIN), 14,493 tangu Disemba 31, 2019, licha ya kuzalishwa na Makao Makuu na kuletewa ofisini kwake Mjini Songea.

Pia Waziri Lugola amemuondoa madarakani Afisa wa NIDA Wilaya ya Namtumbo, Mkoani humo, Thobias Nangalaba kwa uzembe wa kutofika katika kikao chake cha viongozi wa Mkoa na Wilaya, licha ya kupewa taarifa ya kuhudhuria kikao hicho.

Akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika Viwanja vya Soko Kuu la Manispaa ya Songea Mkoani humo, leo, Waziri Lugola amesema, amewatengua vyeo
maafisa wawili hao kwa kucheza na kazi za Serikali, kwa kutojali majukumu yao.

“Ndugu wananchi wa Songea, maafisa hawa wamekuwa wakienda kinyume na maagizo ya Serikali la kuwataka waweze kuwakamilishia wananchi usajili wa laini za simu kwa alama za vidole kwa wakati, hivyo hawatufai na wanapaswa watupishe ili wengine waweze kuiongoza NIDA Mkoani hapa, haiwezekani Afisa wa NIDA Mkoa anacheza na wananchi kwa kutopeleka taarifa ili waweze kupata fursa ya kusajili laini zao  ambapo zoezi hilo linatarajia kukamilika Januari 20 mwaka huu,” alisema Lugola.

Alisema Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais Dkt. John Pombe Magufuli inawajali wanyonge hivyo yeye Waziri wa Mambo ya Ndani ya Ndani ya Nchi, anapambana na watu wanaokwamisha jitihada za Serikali.

Aidha, Waziri Lugola aliitaka Idara ya Uhamiaji Mkoani humo kufanya kazi usiku na mchana wakishirikiana na Jeshi la Polisi kuwasaka wahamiaji haramu hasa katika eneo la mpaka wa Tanzania na Msumbiji Mkoani humo.

“Ndugu wananchi, toeni taarifa za wahamiaji haramu, itasaidia kuwakamata na pia kuwashughulikia ipasavyo kwakuwa watu hao ni hatari kwa uhalifu,” alisema Lugola.

Aliongeza kuwa, Jeshi la Polisi lipo imara na linaendelea kulinda usalama wan chi, matukio ya uhalifu makubwa yamesambaratishwa, na matukio yaliyobaki ni madogo
ambayo hayana nguvu katika amani ya nchi.

“Serikali ya Dkt. John Pombe Magufuli ipo imara, uhalifu sasa haupo, ujambazi tumeusambaratisha kabisa, kama kuna uhalifu basi mdogo mdogo tu, huyu kanitukana hivi na vile lakini matukio ya uhalifu makubwa hayapo nchini, nyie mashahidi na mnaona,” alisema Lugola.

Waziri Lugola anaendelea na ziara yake baada ya kumaliza Mkoa wa Ruvuma, anatarajia kwenda Mtwara na Mkoa wa Lindi.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527