WAFUNGWA 136 WAACHIWA HURU SIMIYU KUFUATIA MSAMAHA WA RAIS, WAAHIDI KUWA RAIA WEMA

Na Stella Kalinga, Simiyu

Jumla ya wafungwa 136 kutoka magereza za Mkoa wa Simiyu wamechiwa huru kufuatia msamaha wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John  Pombe  Magufuli alioutoka Desemba, 2019 katika sherehe za maadhimisho ya miaka 58 ya Uhuru wa Tanzania Bara yaliyofanyika jijini Mwanza.


Akitoa taarifa hiyo mbele ya waandishi wa habari Desemba 10, 2019 Mkuu wa Jeshi la Magereza Mkoa wa Simiyu, ACP. Andulile Mwasampeta amesema  anamshukuru Mhe. Rais Magufuli  kitendo hicho cha kutoa msamaha ambacho kimesaidia kupunguza msongamano kwenye magereza ya mkoa wa Simiyu.

“Ninamshukuru sana Mhe. Rais Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama kwa kutoa msamaha huu ambao umepunguza msongamano katika magereza yetu hususani gereza la Bariadi; nitumie nafasi kuwaasa wafungwa waliosamehewa kwenda kuwa raia wema na wakafanye kazi halali na wasifanye makosa yatakayowaleta tena hapa gerezani,” alisema ACP Mwasampeta

ACP Mwasampeta ameongeza kuwa wafungwa 136 waliopata msamaha wa Rais katika mkoa wa Simiyu ni wale waliokuwa wamebakisha muda wa  siku moja hadi miezi sita miezi 12 kumaliza muda wa vifungo vyao, ambapo amebainisha kuwa wamezingatia maelekezo ya Mhe. Rais katika vigezo vya watu walioachiwa huru.

Aidha, Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka kwa kufanikisha zoezi la kuwaleta pamoja wafungwa wote waliopata msamaha wa  Rais kwa kutoa magari  yaliyowezesha jeshi la magereza kuwachukua katika magereza mbalimbali mkoani Simiyu na kuwaleta katika gereza la Bariadi ambapo ndipo walipoanzia safari ya kurejea majumbani kwao.

Kwa upande wao wafungwa waliopata msamaha wa Rais na kuachiwa huru wamemshukuru Mhe. Rais Magufuli kwa kutoa msamaha huo na kuahidi kuwa raia wema watakaofanya kazi halali na kujiepusha na makosa yote yanayoweza kusababisha wakarudi tena gerezani.

“Namshukuru sana Mhe. Rais kwa msamaha huu alioutoa kwa wafungwa zaidi ya 5000 tuliokuwa magereza mbalimbali niseme tu kwamba wale wote waliokuwa wafungwa kama mimi na wakapata msamaha huu tukawe raia wema na tukachape kazi tujenge nchi yetu, “ alisema Buluba George miongoni mwa wafungwa 136 mkoani Simiyu

“Mimi naahidi kwenda kujishughulisha na shughuli za kuniwezesha kupata kipato, nitajitahidi kufanya kazi kwa bidii ili nisije nikaletwa tena huku gerezani, namshukuru sana Rais Magufuli kwa kutupa msamaha huu,” alisema Musa Lazaro miongoni mwa wafungwa 136 mkoani Simiyu

MWISHO



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527