MARUFUKU UCHIMBAJI HOLELA WA MADINI YA UJENZI KAHAMA

NA SALVATORY NTANDU

Wachimbaji na wamiliki wa maeneo yenye  madini ya ujenzi wilayani kahama mkoani Shinyanga wametakiwa kuwa leseni za uchimbaji ambazo zitawasaidia kuepukana na kutaifishwa kwa madini hayo pindi yanapokamatwa  na kubainika kutolipiwa kodi ya serikali.

Kauli hiyo imetolewa jana na Kamishina wa madini wa mkoa wa Shinyanga Mhandisi Joseph Kumburu kwenye mkutano maalumu na wamiliki wa maeneo ya uchimbaji, wachimbaji, wasafirishaji mjini kahama kuhusiana na kuwa na leseni za uchimbaji wa madini ya Ujenzi.

Amesema kwa mujibu wa sheria ya Madini ya mwaka 2010 kifungu cha sita na marekebisho ya kifungu cha 30 ni kosa la kufanya shughuli za madini bila kibali hivyo wanapaswa kuwa na leseni na hawatakubali kuendelea na  uchimbaji holela wa madini ya ujenzi katika mji wa kahama.

“Tumekuja kutoa elimu kwa kundi hilo linalojihusisha na shughuli za madini ili waitambue sheria hii na namna inavyofanya kazi endapo tukiacha uchimbaji huu holela ukaendelea katika wilaya ya kahama maeneo mengi yatabaki kuwa na mashimo”alisema Kumburu.

Naye mwenyekiti wa Wachimbaji wa madini ya Ujenzi katika wilaya ya kahama Martine Clemency amesema bado wanakabiliwa na changamoto nyingi katika uchimbaji wa madini hayo kutokana na mrundikano wa tozo pindi wanaposafirisha madini ya ujenzi.

“Msafirishaji wa madini haya anatozwa kodi shilingi 2500 kwa kila gari na wakati mwingine hutozwa zaidi ya mara mbili kutokana na kuwepo kwa mageti mengi kabla ya kufikisha mzigo kwa mteja wake jambo ambalo limekuwa likisababisha usumbufu kwa madereva wangu”alisema Martine.

Kwa upande wake ofisa Mazingira wa halamshauri ya mji wa Kahama Johanes Mwebesa amesema halamshauri ya mji imetenga maeneo ya uchimbaji wa madini katika kata ya Ngogwa  na wachimbaji wote wa madini ya Ujenzi waliopo mjini watalazimika kwenda huko ili kuzuia uharibifu wa mazingira.

“Tumefanya tahimini na kujiridhisha kuwa maeneo ambayo tumeyatenga yanafaa kwaajili ya shughuli hizo na muda si mrefu mtalazimika kwenda huko na kuondoka hapa mjini kwaajili ya shughuli hizo za uchimbaji madini Ujenzi”alisema Mwebesa.

Mkutano huo umejumusha wachimbaji,wamiliki wa magari na madereva wapatao 100 na madini ujenzi ambayo yanapaswa kulipiwa ushuru ni pamoja na kokoto,mchanga na moramu.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527