WAZIRI UMMY ASEMA SERIKALI INAENDELEA NA MCHAKATO WA KUBORESHA SERA MPYA YA AFYA

Na.Faustine Gimu Galafoni.Dodoma

Waziri wa afya maendeleo ya jamii jinsia wazee na watoto Mhe. Ummy mwalimu amesema serikali inaendelea na mchakato wa kuboresha sera mpya ya afya  ili kuimarisha huduma  za afya nchini badala ya kuendelea na sera iliyopo kwasasa ambayo imepitwa na wakati.

Waziri Ummy amesema hayo  jana Nov.27,2019 jijini Dodoma wakati akifungua Kongamano  la sita la   afya nchini  lijulikanalo  “TANZANIA HEALTH SUMMIT “ambapo pamoja na mambo mengine ameendelea kusisitiza  dhamira yake ya kuwasilisha bungeni muswaada utakao lazimisha kila mtanzania kuwa na bima ya Afya.

Waziri Ummy amesema Sera ya Afya ya Mwaka 2017 imejikita zaidi katika masuala ya tiba na si kinga hivyo Sera Mpya ya mwaka 2019/2020 itajikita zaidi katika Masuala ya kinga kwani kinga ni bora kuliko tiba.

Aidha ,Waziri Ummy amesema katika sera Mpya ya Afya ya Mwaka 2019/2020 itaangalia mktadha wa kuwafikia wananchi huduma ya Afya yaani Afya kwa wote kwa kuangalia vigezo muhimu vya uhitaji  tofauti ya na sera ya iliyopo ambapo inasema zahanati kila kijiji bila kuangalia mzigo wa Magonjwa ama geografia ya eneo husika.

Kwa upande wake Rais wa Kongamano la Afya nchini Tanzania, Dokta Omary Chillo  amesema Lengo la kongamano hilo ni kujadili changamoto mbalimbali zilizopo katika sekta ya afya na namna ya kukabiliana nazo ili kuleta ufanisi zaidi katika utendaji kazi.

Kongamano la sita la Afya Mwaka 2019 limeanza Nov.27 hadi  28,2019  huku likiandaliwa na Taasisi  sita ambazo ni  Wizara ya Afya Tanzania,Wizara ya Afya  Upande wa Zanzibar ,Ofisi ya Rais TAMISEMI ,Tume ya Huduma za kijamii ya Kikristo,Baraza la Waislam Tanzania[BAKWATA]  na Tindwa Medical Services   na kaulimbiu ni ufanisi na Matokeo katika utoaji wa huduma za Afya.

Mwisho.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527