VIWANDA VYA NGUO, GLASI KUJENGWA BARIADI SIMIYU

Na Stella Kalinga, Simiyu RS

Mwekezaji kutoka  nchini Uturuki, Bw. Mustafa Albayram ameahidi kujenga viwanda viwili; kiwanda cha nguo na kiwanda cha kutengeneza glasi katika eneo la Isanga Mjini Bariadi Mkoani Simiyu mwaka 2020, mara baada ya kuridhishwa na mazingira ya uwekezaji  ambapo viwanda hivyo vinatarajia kuajiri wananchi  takribani 2000.

Albayram ameyasema hayo Novemba 13, 2019 mara baada ya kutembelea maeneo mbalimbali kwa lengo la kuangalia mazingira wezeshi  kwa  uwekezaji wa viwanda, ambaye alifuatana na Balozi wa Tanzania nchini Uturuki, Prof. Elizabeth Kiondo kwa ziara ya siku mbili mkoani Simiyu.

Amesema endapo miundombinu yote muhimu hususani umeme itawekwa kwa wakati katika eneo hilo uwekezaji huo utaanza mara tu baada ya kukamilisha taratibu zote muhimu zinazohitajika ikiwa ni pamoja na usajili wa kampuni na kutafuta hati miliki ya ardhi.

“Tumeamua kuwekeza Simiyu, kila kitu kikienda sawa kiwanda cha nguo kinaweza kujengwa na kufanya kazi ndani ya miezi tisa mpaka mwaka mmoja, kiwanda cha glasi ni mwaka mmoja; baada ya usajili wa kampuni nitarudi tena Simiyu kukamilisha masuala ya hati miliki ya ardhi, sitaki kumuangusha Mhe. Balozi maana amefanya mengi kwa ajili yetu,” alisema Albayram.

Balozi wa Tanzania nchini Uturuki, Prof. Elizabeth Kiondo amesema mwekezaji ameridhishwa na eneo hilo na kuushukuru uongozi wa Mkoa wa Simiyu kwa kutoa ardhi bure huku akibainisha kuwa ombi kubwa la mwekezaji ni kuwa na nishati ya kutosha kwa kuwa viwanda hivyo hususani kiwanda cha nguo.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka amemhakikishia mwekezaji huyo upatikanaji wa mahitaji yote muhimu na kuahidi kushirikiana na taasisi zote za Serikali zinazohusika kuhakikisha anapata huduma zote kwa wakati na bila urasimu wowote.

Kuhusu suala la Umeme Mtaka amesema katika Bajeti ya mwaka 2019/2020 Wizara ya Nishati kupitia Shirika la umeme TANESCO imetenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha kupozea umeme(substation) ambacho kitajengwa karibu na eneo la uwekezaji huo

Mtaka ameongeza kuwa mtazamo wa mkoa wa Simiyu ni kuwa na viwanda vichache vinavyoajiri watu wengi badala ya kuwa na viwanda vingi vinavyoajiri watu wachache, huku akitoa wito kwa wakulima wa pamba kulima pamba kwa wingi kwa kuwa kiwanda cha nguo kitakuwa mkombozi wa kuongeza thamani ya zao la pamba na itauzwa kwa bei ya uhakika.

Naye Katibu wa Chama cha Wanunuzi wa pamba nchini, Bw. Boaz Ogola amesema kujengwa kwa kiwanda cha nguo mkoani Simiyu kutasaidia wakulima wa pamba kupata soko la uhakika kuondoa changamoto ya bei ya pamba kwa kuwa kitapanua wigo wa soko la pamba, ambapo pamba inayotumika hapa ni nchini ni asilimia 20-25 ya pamba yote inayozalishwa.

MWISHO


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527