MKUTANO WA TAASISI ZA FEDHA NCHINI KUFANYIKA ARUSHA NOVEMBA 21 & 22, 2019


Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kwa kushirikiana na Umoja wa Mabenki Tanzania (TBA) imeandaa mkutano wa taasisi za fedha nchini utakaofanyika jijini Arusha kujadili namna ya kuchochea maendeleo ya sekta ya fedha nchini.


Mkutano huo wa 19 wa taasisi za fedha unatarajiwa kufunguliwa na kiongozi wa ngazi ya kitaifa. Utahudhuriwa na washiriki wapatao 300 wakiwemo Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, mawaziri, wakuu wa taasisi za fedha, wachumi wabobezi, wanataaluma na washirika mbalimbali wa maendeleo.

Mada zingine zitakazotolewa na kujadiliwa katika mkutano huo ni pamoja na, ‘Matumizi ya teknolojia katika kukuza sekta ya fedha ili kuleta mapinduzi ya viwanda’; ‘Maeneo yenye fursa za uwekezaji katika sekta ya fedha’ na ‘Vigezo vinavyochangia kujenga tabia za ukopaji’.

Pia, washiriki wa mkutano huo watajadili kuhusu ‘Jinsi ya kukinga vihatarishi katika sekta ya fedha’; ‘Namna ya kuoanisha sekta ya fedha na maendeleo ya viwanda’; na ‘Tathmini ya mchango wa sekta ya benki katika huduma jumuishi za kifedha nchini’.

Benki Kuu ya Tanzania imekuwa ikiandaa mikutano ya taasisi za fedha kila baada ya miaka miwili tangu miaka ya 1980. 

Katika mikutano hii, viongozi wakuu wa taasisi za fedha, yakiwemo mabenki, mashirika ya bima, mifuko ya hifadhi za jamii na taasisi zingine za fedha wamekuwa wakikutana na kujadili masuala mbalimbali kwa ajili ya maendeleo ya sekta ya fedha na uchumi wa nchi kwa ujumla. Mkutano wa 18 wa taasisi za fedha ulifanyika mwaka 2016 jijini Arusha na mada kuu katika mkutano huo ilikuwa ni ‘Jinsi sekta ya fedha inavyoweza kuifanya Tanzania inufaike kiuchumi kutokana na uwepo wake kijiografia’ (Harnessing Tanzania’s Geographical Advantage: The role of financial sector).


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527