MREMA ALALAMIKA KUCHEZEWA RAFU UCHAGUZI SERIKALI ZA MITAA


Mwenyekiti wa chama cha TLP, Augustino Mrema, amesema anaenda kulalamika kwa Rais wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, kwa kile alichokidai mgombea wa chama chake kufanyiwa hujuma, ili mgombea wa Chama Cha Mapinduzi ashinde Uenyekiti wa Serikali za Mitaa katika Kijiji alichozaliwa yeye cha Kiraracha.

Mrema amedai katika zoezi hilo walijitokeza baadhi ya watu, yeye mwenyewe hakuwafahamu walimlazimisha wakala wake kunywa bia, wakati zoezi la kupiga kura likiwa linaendelea huku wakala wake akikataa kufanya hivyo.

"Wananchi wangu walimuona Mwenyekiti wao wa zamani aliyekaa miaka 10 anafaa kuendelea kuwaongoza, nilichoshangaa ni kuwa nguvu kubwa ilitumika, kwa sababu kulikuwa na idadi kubwa ya Polisi na wengine walilazimika kuleta bia ili wakala wangu anywe." Amesema Mrema

"Walipoleta bia, wakala wangu alikataa basi wakatumia hiyo nafasi kufanya mgombea wa chama kingine ashinde nafasi hiyo, kilichonishangaza Vijiji vyote havikukubaliwa wagombea wetu ni Kijiji kimoja tu."

Jana Novemba 24, 2019 Watanzania wa maeneo mbalimbali nchini, walishiriki zoezi la kupiga kura kwa kuwachagua viongozi wa Serikali za Mitaa, Vijiji pamoja na Vitongoji.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527