WATER MISSION TANZANIA YAFANIKISHA MIRADI YA MAJI SALAMA KWENYE KAMBI ZA WAKIMBIZI MKOANI KIGOMA


Mhandisi wa maji kutoka shirika la Water Mission Tanzania, OpitaTarcicous (kushoto) akitoa maelezo kwa ujumbe wa Balozi wa Denmark nchini Mette Nørgaard Dissing-Spandet (katikati) wakati wa uzinduzi wa mradi wa maji salama katika kambi ya wakimbizi ya Nyarugusu mkoani Kigoma mwishoni mwa wiki ambao umetekelezwa na water Mission Tanzania , Poul Due Jensen Foundation, na wadau wengine.
Wakurugenzi kutoka taasisi za water Mission Tanzania , Poul Due Jensen Foundation wakitembelea mind main ya mradi.
Ujumbe wa Balozi wa Denmark nchini na Wakurugenzi wa mashirika ya water Mission Tanzania , Poul Due Jensen Foundation na Water Mission International ukikaribishwa wakati wa hafla ya uzinduzi wa mradi wa maji wa Nyarugusu.

Na Mwandishi WEtu.

Shirika la kimataifa lisilo la Kiserikali la Water Mission Tanzania, linaendelea kuwanufaisha watu kwenye maeneo yenye shida ya maji nchini kwa kutekeleza miradi ya kuwapatia maji salama ikiwemo maeneo ya kambi ya Nyarugusu, mkoani Kigoma.

Water Mission Tanzania, imekuwa ikitekeleza miradi yake kwa kushirikiana na taasisi za Poul Due Jensen Foundation, Grundfos Corporation, UNHCR, Wizara ya Maji na Wizara ya Mambo ya Ndani, kuhakikisha kambi za wakimbizi Tanzania zinakuwa na uhakika wa kupata maji salama.

Mbali na miradi ya maji kwenye kambi za wakimbizi mkoani Kigoma, Tanzania, Water mission Tanzania, imetekeleza miradi ya maji ipatayo 24 katika maeneo mbalimbali ya vijijini nchini yenye changamoto ya kupata maji safi, tangu ilipoanza kutoa huduma zake nchini mnamo mwaka 2014.

Hadi leo hii, wenyeji 30,000 wa Zeze, Kasanda, Kakonko, Heru Ushingo, Mvugwe na Kazilamihunda-Juhudi wanapata maji safi na salama. Katika siku zijazo, Water Mission Tanzania na washirika wake wanatumai kuwahudumia hadi watu 80,000 katika jamii zinazozunguka kambi nchini Tanzania kwa kujenga miradi ya maji safi na salama.

Akiongea wakati wa hafla ya uzinduzi wa mradi wa maji wenye uwezo wa KW 100 kupitia nguvu ya jua katika kambi ya wakimbizi ya Nyarugusu mkoani Kigoma, Balozi wa Denmark nchini, Mette Nørgaard Dissing-Spandet, amepongeza mpango huu wa ushirikiano wa mashirika yasiyo ya serikali na Serikali katika kukabiliana na changamoto katika jamii kama kufanikisha miradi ya kusaidia jamii kama miradi ya maji .

Mkurugenzi Mkuu wa taasisi ya The Grundfos Foundation (Poul Due Jensen Foundation), Kim Nøhr Skibsted amesema, ”Mradi huu ulianza kufanyiwa kazi mwaka 2016 wakati taasisi za Grundfos Foundation na Water Mission zilipodhamiria kuondoa miundo mbinu ya mradi wa zamani uliokuwepo na kujenga mradi unaotumia teknolojia za kisasa na umeme wa jua, lengo likiwa ni kuwapatia maji safi na salama maelfu ya wakimbizi kwenye kambi ya Nyarugusu na maeneo ya vijiji jirani”.

Skibsted, ameongeza kusema kuwa mradi huu ni wa pekee miongoni mwa miradi ya maji iliyotekelezwa na taasisi hiyo kwa kuwa mbali na kuwezesha jamii kupata maji safi zinawezeshwa kupata maarifa ya kutunza mradi na matumizi ya nishati mbadala kuendesha miundombinu yake “Mfumo wa ushirikiano wa wadau kufanikisha miradi kwa maeneo yenye mahitaji unapaswa kutumika sehemu mbalimbali duniani kama ambavyo wadau mbalimbali wameshirikiana kuhakikisha eneo hili la wakimbizi wanapata maji salama na kuondoa hatari ya milipuko ya magonjwa yatokanayo na ukosefu wa maji salama”,alisisitiza.

Naye Makamu wa Rais wa miradi ya kimataifa kutoka Water Mission International, Bw. Seth Womble, amesema kuwa kufanikisha kwa miradi ya maji katika makambi ya wakimbizi kumewaongezea kujiamini katika utekelezaji katika maeneo mengine nchini na kanda nzima “Ushirikiano wetu na wadau wengine unadhihirisha jinsi unavyoweza kufanikisha miradi kwenye maeneo mengine yenye changamoto maji salama kama ilivyo dira ya shirika la Water Mission”.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527