WALENGWA WA TASAF WILAYANI RUNGWE WAISHUKURU SERIKALI KWA KUWAKUMBUKA


 Baadhi ya Wajumbe wa Kamati ya Uongozi ya Taifa ya TASAF wakipata maelezo ya namna chanzo cha maji kilichojengwa katika eneo la Bulyaga Juu ,nje kidogo ya mji wa Tukuyu kilivyojengwa kupitia utaratibu wa Ajira ya Muda unaotekelezwa na Serikali kupitia TASAF.Maji hayo hayakauki katika kipindi chote cha mwaka.
 Mmoja wa Wajumbe wa Kamati ya Uongozi ya Taifa ya TASAF,Dkt. Naftal Ng’ondi (mwenye kote cheupe) akimtwisha ndoo ya maji mmoja wa Walengwa wa TASAF katika chanzo cha maji kilichojengwa wa TASAF katika eneo la Bulyaga juu ,halmashauri ya Rungwe kwa utaratibu wa Ajira ya Muda.
 Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF,Ladislaus Mwamanga (aliyeinama) akigusa maji kwenye chanzo cha maji kilichojengwa na Walengwa wa TASAF katika eneo la Bulyaga juu, nje kidogo ya mji wa Tukuyu kupitia utaratibu wa Ajira ya Muda.
Mkuu wa mkoa wa Mbeya Bw. Albert Chalamila (aliyevaa suti ya bluu) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wajumbe wa kamati ya uongozi waTaifa ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii -TASAF na menejimenti ya Mfuko huo baada ya kukamilisha mazungumzo ofisini kwake. Wa kwanza kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF ,Bw. Ladislaus Mwamanga.

                                                   **
Na Estom Sanga- RUNGWE. 

Kamati ya Uongozi ya Taifa ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii –TASAF imefanya ziara katika Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe Mkoani Mbeya kukagua miradi inayotekelezwa na Mfuko huo na kuonyesha kuridhishwa kwake na mafanikio makubwa yaliyopatikana kupitia Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini . 

Kabla ya kutembelea halmashauri ya Wilaya ya Rungwe, Wajumbe wa Kamati hiyo ya Uongozi ya Taifa ya TASAF,walikutana na Mkuu wa mkoa wa Mbeya ,Bw. Albert Chalamila ambaye amewaeleza wajumbe hao kuwa utekelezaji wa miradi ya TASAF mkoani humo imeleta hamasa kubwa kwa wananchi kuuchukia umaskini kwa kufanyakazi kwa bidii. 

Mkuu huyo wa mkoa wa Mbeya amesema licha ya utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini kutotekelezwa katika baadhi ya maeneo ya mkoa huo,mafanikio yake yamesababisha wananchi ambao hawajafikiwa na huduma za Mpango huo kuomba wajumuishwe ili nao waweze kunufaika na utaratibu huo wa serikali wa kuzifikia kaya maskini. 

Aidha Bw. Chalamila amesema sekta za elimu, afya,na shughuli za uzalishaji mali vimepata msukumo mkubwa kwa kaya za Walengwa wa TASAF ambao kabla ya kuanza kwa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini waliishi katika hali ya unyonge uliosababishwa na umaskini wa kipato jambo ambalo amesema limepungua kwa kiwango kikubwa baada ya Serikali kupitia TASAF kuanza kutekeleza Mpango huo. 

Wakiwa Katika halmashauri ya wilaya Rungwe,Wajumbe wa Kamati hiyo ya Uongozi ya taifa ya TASAF wamepata fursa ya kukutana na baadhi ya Wananchi wanaonufaika na huduma za Mfuko huo ambao wameonyesha baadhi ya mafanikio waliyopata hususani katika sekta ya uboreshaji wa makazi, elimu,afya na huduma ya maji ambayo wamesema umewasaidia kuboresha maisha yao na kuwapa hamasa kubwa ya kukabiliana na umaskini. 

Akizungumza kwa nyakati tofauti katika ziara hiyo,Kaimu Mwenyekiti wa kamati hiyo Dr. Naftal Ng’ondi amewahimiza walengwa wa TASAF kutumia vizuri fursa hiyo ili waweze kuunga mkono jitihada za serikali za kuondoa kero ya umaskini miongoni mwao,kwani amesema mkakati huo unapaswa kuwa wa muda ili waweze kupisha wananchi wengine waweze kunufaika nao. 

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF, Bw. Ladislaus Mwamanga akijibu hoja ambayo imekuwa ikiibuliwa na wananchi katika maeneo ambayo hayakujumuishwa kwenye huduma za Mpango, amesema serikali imeamua katika sehemu ya pili ya Mpango wa kunusuru Kaya Maskini maeneo yote nchini yajumuishwe kwenye huduma za Mpango huo. 

Bwana Mwamanga amesema uamuzi huo wa serikali ambao unaweka msisitizo kwa Wananchi watakaojumuishwa kwenye Mpango kufanyakazi za maendeleo watakazozibua kwenye maeneo yao na kisha kulipwa ujira kwa kazi hizo jambo ambalo amesema litachangia kuboresha maisha yao. Hata hivyo amefafanua kuwa Walengwa ambao ni wazee , wagongwa wa muda mrefu, watoto yatima na walemavu ambao hawana msaada wataendelea kupata huduma za uhawilishaji fedha ili waweze kujikimu .

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527