WAZIRI MABULA AKEMEA UCHELEWESHAJI UTOAJI HATI ZA ARDHI

Na Munir Shemweta, WANMM TABORA

Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula amekemea ucheleweshaji utoaji Hati za Ardhi katika Manispaa ya Halmashauri ya Tabora mkoani Tabora na kueleza kuwa hali hiyo inachangia kuikosesha serikali mapato yatokanayo na kodi ya ardhi.

Dkt Mabula alitoa kauli hiyo tarehe 13 Agosti 2019 wakati wa ziara yake ya kuhamasisha ukusanyaji maduhuli ya serikali kupitia kodi ya ardhi pamoja na kukagua mifumo ya kodi kwa njia ya kielektronik na Masijala ya ardhi katika mkoa wa Tabora.

Kauli ya Naibu Waziri wa Ardhi inafuatia kubaini uwepo Hati za Ardhi 92 katika Manispaa hiyo ambazo hazijafanyiwa kazi kwa muda mrefu kwa maelezo kuwa baadhi ya majalada ya hati hizo yalikuwa na upungufu na wahusika wake hawapatikani.

Dkt Mabula alishangazwa na hali hiyo kwa kuwa baadhi ya maombi ya Hati za Ardhi yana zaidi ya miaka miwili katika Ofisi ya Afisa Ardhi Mteule wa Manispaa ya Tabora tangu mwaka 2016 bila kufanyiwa kazi jambo alilolieleza kuwa linawakatisha tamaa wananchi wanaoomba Hati.

Kufuatia hali hiyo, Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula alimuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Tabora Bosco Ndunguru kumuandikia barua ya onyo Afisa Ardhi Mteule wa Daudi Msengi kwa kushindwa kuwajibika ipasavyo.

Kwa mujibu wa Dkt Mabula, kwa sasa Wizara yake haitamvumilia Mtumishi yeyote wa sekta ya ardhi atakayeshindwa kutekeleza majukumu yake na kusisitiza kuwa kuwa  upandishwaji vyeo kwa watmushi utazingatia utendaji kazi na kuwataka kuacha kufanya kazi kwa mazoea.

Amezitaka Halmashauri nchini kupanga malengo ya uandaaji Hati za Ardhi kwa watendaji wake ili kuelewa kwa siku moja zinaandaliwa Hati ngapi na kufafanua kuwa hiyo itazisaidia halmashauri kufikia malengo ya utoaji hati. Dkt Mabula alitolea mfano wa halmashauri ya Ilemela mkoani Mwanza kuwa imejiwekea malengo ya kuandaa hati tano kwa siku moja jambo lililoiwezesha kuandaa hati nyingi na hivyo kuwa moja ya halmashauri inayofanya vizuri kwa utoaji Hati za Ardhi.

Dkt Mabula alisema, manispaa ya Tabora imeshindwa hata kutimiza malengo yake ya kutoa hati katika mwaka wa fedha 2018/2019 ambapo Manispaa hiyo ilijiwekea kutoa jumla ya Hati 2000 lakini ilifanikiwa kutoa 1200 tu.

Aidha, alitaka suala la kuandaa Hati za Ardhi lifanywe na Maafisa Ardhi kwa kuwa wote wana taaluma ya ardhi badala ya kumtegemea Afisa Ardhi Mteule ambaye wakati mwingine  amekuwa akichelewesha kwa kisingizio cha kutingwa na shughuli nyingi.

Ameitaka Manispaa ya Tabora kuongeza kasi ya utoaji Hati za Ardhi kwa wananchi  katika Manispaa hiyo ili kuwamilikisha na kuchangia mapato ya serikali kupitia kodi ya ardhi sambamba na kuhimiza Maafisa Ardhi kuwa na kauli nzuri kwa wateja  kwa lengo la kujenga mazingira mazuri ya utendaji.

Katika hatua nyingine Naibu Waziri wa Ardhi nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula amewakabidhi wananchi kumi na tano wa eneo la Uledi katika Kata ya Mpera mkoani Tabora Hati za Ardhi kwa niaba ya wenzao takriban 2117 baada ya kukamilisha taratibu za kupatiwa hati.

Dkt Mabula alisema usalama wa miliki ya ardhi ni kupatiwa Hati ya Ardhi na kusisitiza usalama wa eneo siyo kuwekewa Beacons pekee bali wananchi wanahitaji kupatiwa hati ili ziweze kuwasaidia katika shughuli za uchumi ikiwemo kuchukua mikopo benki.

Ameagiza kukamatwa kwa wale wote waliohujumu alama za mipaka katika maeneo ya ardhi eneo la Uledi kwa kung’oa Beacons na kusisitiza kuwa hakuna mtu aliye juu ya sheria na wote waliofanya kosa hilo wachukuliwe hatua ikiwemo kufikishwa katika vyombo vya sheria

Kamishna Msaidizi wa Ardhi Kanda ya Magharibi Idrisa Kayera alisema upimaji ardhi katika Manispaa ya Tabora kwa sasa umeongezeka tofauti na miaka ya nyuma ambapo maeneo mengi yanapimwa na kupangwa na kubainisha kuwa ofisi yake itahakikisha wananchi wanamilikishwa na kueleza kila mwananchi mwenye eneo kufuatilia taratibu za kumilikishwa.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527