HALMASHAURI KUU CCM NJOMBE YATOA MAAGIZO HAYA KWA SERIKALI

Na Amiri kilagalila-Njombe

Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Njombe imetoa maelekezo kwa mkuu wa mkoa wa Njombe na Mkuu wa Wilaya ya Njombe kukutana haraka iwekezanavyo na wadau wa usafirishaji wa abiria mkoani humo ili kutatua changamoto inayowakumba wananchi wanaosafiri kwa mabasi kushindwa kushushwa  katikati ya mji wa Njombe baada ya stendi kuu mpya kuanza kufanya kazi.

Akizungumzia baadhi maazimio ya kikao cha  halmashauri kuu ya CCM mkoa wa Njombe iliyokutana siku chache zilizopita na kujadili utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya CCM ya Mwaka 2015/2020 kwa mwaka wa fedha 2018/19, katibu wa siasa na uenezi wa CCM mkoa wa Njombe, Erasto Ngole amesema CCM imesikia kilio cha wananchi juu ya adha wanayoipata abiria wanaposhindwa kushushwa na mabasi ya abiria katikati ya mji na hivyo imeagiza lazima kuwepo na kituo cha mabasi katikati ya mji wa Njombe.

“Chama cha mapinduzi mkoa wa Njombe tumempa maelekezo mkuu wa mkoa pamoja na mkuu wa wilaya na mkurugenzi wa halmashauri ya mji waite mkutano mkubwa wa wadau wanaohusika na usafiri,ili waweze kuangalia namna bora ya kuondoa haya manung’uniko,na sisi tumetoa mapendekezo kati kati ya mji lazima kuwe na kituo cha kushusha na kupakia abiria,haiwezekani kabisa mwananchi akapitishwa mjini kusiwe na kituo hata kimoja”alisema Ngole

Katika hatua nyingine kuhusu swala la vitambulisho vya ujasiriamali amesema chama kimetoa maelekezo  kwa serikali ya mkoa wa Njombe kuzingatia utaratibu wa ugawaji wa vitamburisho hivyo.

“Imeonekana kwa sasa yameorodheshwa makundi mbalimbali na watu wanagawiwa vitambulisho ili viishe,mheshimiwa Rais alisema wanaotakiwa kuwa na vitambulisho ni wafanyabiashara wadogo wadogo wenye mauzo chini ya milioni nne kwa mwaka kwa hiyo ni lazima tuzingatie hilo na halmashauri kuu ya mkoa imekazia hilo”aliongeza Ngole

Aidha kuhusu ujenzi wa barabara ya kiwango cha lami kutoka Njombe kuelekea tarafa ya Lupembe hadi mpakani na mkoa wa Morogoro, Ngole amesema chama cha mapinduzi kimeitaka serikali kuanza ujenzi wa barabara hiyo mara moja kwa sababu wananchi wanaoishi maeno hayo wamekuwa wakipata adha kubwa ya usafiri kutokana na miundombinu ya barabara kuwa mibovu.

Kwa upande wake mwenyekiti wa jumuia ya umoja wa vijana mkoa wa Njombe (UVCCM) Nehemia Tweve ametoa wito kwa vijana kuona fulsa mbali mbali zilizopo katika mkoa huo ikiwemo utalii licha ya kilimo na ufugaji ambazo zimezoeleka na wengi




Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527