WANANE WAKAMATWA WAKITAKA KUMTOA KAFARA MTOTO KWA MGANGA WA KIENYEJI

Jeshi la Polisi Mkoani Ruvuma linawashikilia watuhumiwa wanane wakiwemo wanne wa kutoka mkoani Njombe wakitaka kumtoa mtoto mdogo kafara katika mlima Mgwijima wilayani Namtumbo kwa mganga Faraji Panjapi.

Watuhumiwa hao, wanne kutoka mkoani Njombe na wanne kutoka mkoani Ruvuma wanashikiliwa na Polisi wilayani Namtumbo kwa kufanya ramli chonganishi na kutaka kumtoa kafara mtoto mdogo.

Walikamatwa katika Mlima Mgwijima wakiwa na mtoto mdogo  na vifaa mbalimbali vinavyodaiwa kutumika katika kafara wakiwemo mbuzi mmoja mweusi, kuku wawili (mmoja mweusi na mwingine mweupe).

Inadaiwa Polisi baada ya kupata taarifa za kiintelijensia walifika katika mlima huo na kuwakamata watuhumiwa hao ikiwa ni pamoja na mganga wa kienyeji, lakini baada ya mahojiano walikana madai hayo.

Awali, mmoja wa watuhumiwa, mwanamke ambaye alikuwa na  mtoto huyo akiwa ametokea Njombe, baada ya kufika kituo cha polisi  ‘alipandisha mashetani’ na kuanza kujigaragaza akisema wale wengine hawana makosa ila yeye.

Baadaye alipotulia na kuhojiwa alikana madai hayo na kudai kuwa yeye ni mgonjwa, hivyo alioteshwa kutoka Njombe kwenda kwenye mlima huo ili kupona. Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi wa tukio hilo.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527