WIZARA YA MAJI YAOMBA KUTENGEWA SH634.19 BILIONI KATIKA BAJETI YAKE YA MWAKA WA FEDHA 2019/2020


Waziri wa wizara ya maji, Profesa Makame Mbarawa amewasilisha mapendekezo ya  kutengewa Sh634.19 bilioni katika bajeti yake ya mwaka wa fedha 2019/2020.

Ametoa mapendekezo hayo leo   Alhamisi  Mei 2 bungeni jijini Dodoma akitaka Bunge kuridhia mapendekezo hayo ili kuiwezesha kutekeleza malengo na miradi ya kipaumbele.

Katika fedha hizo, waziri huyo amesema Sh23.72 bilioni ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na Sh610.46 bilioni zitaelekezwa kwenye miradi ya maendeleo. Katika fedha za miradi, amesema asilimia 57 zitatokana na vyanzo vya ndani na asilimia 43 zitatoka nje.

“Katika fedha za matumizi, Sh17.45 bilioni zitatumika kulipa mishahara ya watumishi wa wizara na chuo cha maji na Sh6.26 bilioni kwa ajili ya matumizi mengineyo,” amesema Profesa Mbarawa.

Akitoa taarifa ya utekelezaji wa bajeti ya mwaka 2018/2019  ya Sh697.57 bilioni, amesema hadi Aprili 2019 wizara ilikuwa imepokea Sh16.65 bilioni sawa na asilimia 68 ya Sh24.36 bilioni zilizotengwa kwa matumizi ya kawaida na Sh343.48 bilioni sawa na asilimia 51 ya Sh673.21 bilioni kwa ajili ya miradi ya maendeleo.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post