BABA AFIKISHWA MAHAKAMANI KWA KUMCHOMA MWANAE PANGA LA MOTO

Picha haihusiani na habari hapa chini
Mkazi wa mtaa wa Fisi, kata ya Igunga mjini mkoani Tabora, Nyalagi Simon amefikishwa katika mahakama ya hakimu mkazi Igunga kwa tuhuma za kumuunguza mwanae kwa upanga wa moto.

Simon amefikishwa leo Jumatatu Aprili 1, 2019 katika mahakama hiyo mbele ya hakimu mkazi mfawidhi wa wilaya, Lydia Ilunda.

Mwendesha mashtaka wa Polisi, Ellymajid Kweyamba alisema mshitakiwa alitenda kosa hilo saa tatu usiku Machi 17, 2019.

Amesema siku hiyo, mshitakiwa akiwa baba wa mtoto (jina linahifadhiwa) alimfanyia vitendo vya ukatili kwa kutumia upanga aliouweka kwenye moto.

Amebainisha kwamba mshitakiwa alikuwa akiutoa upanga kwenye moto na kumuunguza kwenye miguu yote miwili.

Mshitakiwa amekana shitaka lake na amepelekwa mahabusu hadi Aprili 14, 2019 shauri lake litakapotajwa tena.

Na Robert Kakwesi, mwananchi 

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527