Picha : AGPAHI YAENDESHA WARSHA KWA MAMA RIKA MKOA WA MWANZA

Mwezeshaji wa Kitaifa wa Masuala ya Vijana, VVU na UKIMWI, Dk. Happiness Wimile Mbeyela.

Ariel Glaser Pediatric AIDS Healthcare Initiative (AGPAHI) ambayo ni asasi ya kitaifa isiyo ya kiserikali inayojihusisha na mapambano dhidi ya Virusi Vya UKIMWI na UKIMWI imeendesha warsha kwa MAMA RIKA mkoa wa Mwanza ili kuwajengea uwezo kuhusu masuala mbalimbali ya Virusi vya UKIMWI (VVU) na UKIMWI. 


MAMA RIKA ni Waelimishaji wa akina mama wajawazito na wanaonyonyesha wenye maambukizi ya VVU ambao wanapata huduma za tiba na matunzo katika kliniki za kuzuia maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto (PMTCT).

Warsha hiyo ya siku mbili iliyoanza Aprili 24,2019 inafanyika katika ukumbi wa Gold Crest Hoteli Jijini Mwanza na kukutanisha pamoja MAMA RIKA 70 kutoka halmashauri za wilaya mkoa wa Mwanza pamoja na wauguzi, waratibu wa huduma ya afya ya uzazi,waratibu wa huduma za VVU na UKIMWI katika jamii. 

Mwezeshaji wa Kitaifa wa Masuala ya Vijana, VVU na UKIMWI, Dk. Happiness Wimile Mbeyela alisema lengo la warsha hiyo ni kuwajengea uwezo kuhusu masuala ya VVU na UKIMWI hususani uzuiaji wa maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto. 

“Tupo hapa kwa ajili ya kuwajengea uwezo akina mama wanaoishi na VVU kuhusu masuala ya VVU na UKIMWI ili wakatoe elimu kwa akina mama wengine ili wafike kwenye vituo vya afya wanapokuwa wajawazito”,alisema Dk. Mbeyela. 

“Tunawapa ujuzi wa kupigana na unyanyapaa,umuhimu wa kujiweka wazi,jinsi ya kunyonyesha na kuwa wafuasi wazuri wa dawa za kupunguza makali ya VVU (ARVs)
,akina mama hawa watakwenda kutoa elimu kwa akina mama wengine na kuwasisitiza wajiunge kwenye vikundi”,aliongeza Dk. Mbeyela. 

Kwa upande wake,Mwezeshaji katika warsha hiyo, Edwiga Zumba alitoa wito kwa akina mama wajawazito kufika kwenye vituo vya afya na wanapobainika kuwa na maambukizi ya VVU waanze tiba kwa ajili ya kuwakinga watoto wasipate maambukizi ya VVU. 

“Akina mama hudhurieni kliniki,nendeni mkajifungulie hospitali,huko kuna wataalamu wa afya waliobobea ili kupunguza idadi ya watoto wanaozaliwa na VVU kwani maambukizi hutokea wakati wa ujauzito,kujifungua na wakati wa kunyonyesha”,alisema Zumba. 

Nao washiriki wa warsha hiyo,walisema bado kuna changamoto ya baadhi ya akina mama kutokubali kuwa wana maambukizi ya VVU licha ya vipimo kuonyesha kuwa wamepata maambukizi. 

“Tukubaliane na hali,kama umeonekana una maambukizi ya VVU,anza kutumia dawa za ARVs na endelea kupima badala ya kuacha kutumia dawa kwani ukipuuzia utajikuta unazaa mtoto mwenye maambukizi matokeo yake mtoto huyo atakulalamikia kuwa ulimwambukiza kwa maksudi”,alieleza Amina Khamis kituo cha afya Igoma.

ANGALIA PICHA HAPA CHINI
Mwezeshaji wa Kitaifa wa Masuala ya Vijana, VVU na UKIMWI, Dk. Happiness Wimile Mbeyela akizungumza wakati wa warsha kwa MAMA RIKA mkoa wa Mwanza ili kuwajengea uwezo kuhusu masuala mbalimbali ya Virusi vya UKIMWI na UKIMWI katika ukumbi wa Gold Crest Hoteli jijini Mwanza.Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog.
Dk. Happiness Wimile Mbeyela akiwasisitiza akina mama kuwa wafuasi wazuri wa dawa za ARVs.
Dk. Happiness Wimile Mbeyela akielezea kuhusu maana ya VVU na UKIMWI.
MAMA RIKA wakiwa ukumbini.
Dk. Happiness Wimile Mbeyela akizungumza wakati wa warsha hiyo.
Mwezeshaji katika warsha hiyo, Edwiga Zumba akitoa mada kuhusu ufuasi wa dawa za ARVs.
Mwezeshaji katika warsha hiyo, Edwiga Zumba akiwasisitiza akina mama wanaoishi na maambukizi ya VVU wanaonyonyesha kuendelea kutumia dawa za ARVs na kuwashauri wengine kutumia dawa kwani lengo ni kushusha wingi wa VVU na kupandisha CD4 mwilini.
Warsha inaendelea.
Mwezeshaji katika warsha hiyo,Yahaya Isangula ambaye ni Muuguzi kutoka hospitali ya wilaya ya Misungwi akizungumza ukumbini.
Washiriki wa warsha hiyo wakiwa ukumbini.
Amina Khamis kituo cha afya Igoma akichangia hoja wakati wa warsha hiyo.
Washiriki katika warsha hiyo wakiwa ukumbini.
Warsha inaendelea.
Washiriki wa warsha wakifuatilia matukio ukumbini.
Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527