WAZIRI HATAKI MCHEZO..AAGIZA WACHUNGAJI WAKAMATWE TANZANIA



Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Constantine Kanyasu.

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Constantine Kanyasu ametoa agizo kwa maofisa wanyamapori, wanapokamata mifugo itakayokutwa hifadhini, wahakikishe pia wanawakamata wachungaji wa mifugo hiyo.

Amesema hatua hiyo itabadili mfumo wa sasa, ambapo mifugo mingi inayokutwa katika hifadhi imekuwa ikikutwa bila wachungaji huku wengi wakidaiwa kukimbia.

Ametoa agizo hilo wakati akizungumza na mameneja na watumishi wa mapori ya akiba ya Mkungunero na Swagaswaga katika ziara ya kikazi wilayani Kondoa mkoani Dodoma, ambapo amesema shutuma hizo za rushwa zitaisha tu pale watakapokamata mifugo na wachungaji wake.

“Wekeni kambi hapo hapo mahali mtakapoikuta mifugo hadi pale mmiliki wa mifugo au mchungaji atakapojisalimisha awe amejificha na kama amepanda juu ya mti mfuateni, ninyi ni askari tuliowaamini,” amesema Kanyasu.

Ameongeza kuwa, "sitaki kusikia kuanzia sasa eti mmeikamata mifugo bila mchungaji au mmiliki, hakikisheni mnapiga kambi hapo hata ikiwa wiki mbili hadi pale mmiliki atakapojitokeza ili mkamate yeye pamoja na mifugo yake".

Hatua hiyo inakuja kufuatia tuhuma za rushwa zinazowakabili baadhi ya maofisa wanyamapori kuwa baada ya kukamata mifugo hiyo ikiwa hifadhini, huwaruhusu wachungaji wakatafute pesa za kuwahonga ili waiachie, pale wanaposhindwa kupata pesa walizokubaliana, hushindwa kuirudia mifugo yao kwa hofu ya kukamatwa.
Chanzo - EATV

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527