MAANDALIZI YA SHEREHE ZA MEI MOSI YAPAMBA MOTO SOKOINE MBEYA


Waziri wa Nchi Ofisi anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu Mhe. Jenista Mhagama amekagua maandalizi ya Sherehe za Mei Mosi na kusema ameridhishwa na hatua zilizofikiwa.

Ametoa kauli hiyo Aprili 29, 2019 baada ya kupokea taarifa ya mbalimbali za Kamati ya Maandalizi walipokutana kujadili na kupanga mipango katika kuelekea kilele cha sherehe hizo zinazotarajiwa kuadhimishwa katika Viwanja vya Sokoine Jijini Mbeya.

Waziri amesema Kamati ya Mkoa kwa kushirikiana na Ofizi yake imeendelea na maandalizi hayo na kuendelea kutoa wito kwa wananchi wa Mkoa huo kufika kwa wingi katika viwanja hivyo siku ya tarehe 1 Mei, 2019.

“Hadi sasa maandalzi yamefikia hatua nzuri na watu wanafanya kazi kwa umoja ili kuhakikisha shughuli hii inafana, wito wangu wananchi wajitokeze kwa wingi kuja kuunga mkono wafanyakazi wa Tanzania katika siku yao hii muhimu.”Alisema waziri Mhagama.

Waziri aliwataka wanakamati hao wahakikishe wanasimamia vizuri wageni, pamoja na shughuli zote zitakazofanyika uwanjani hapo ili kuhakikisha wanaifikia siku hiyo kwa ushindi mkubwa.

Aidha Waziri aliongezea kuwa, uwepo wa maadhimisho hayo Jijini Mbeya wanachi wayatumie kama fursa ya kimaendeleo kwa kuwa mkoa utapokea wageni wengi hivyo waendelee kuwahudumia vyema.

Aidha kwa Upande wake rais wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (TUCTA) Bw. Tumaini Nyamhokya aliendelea kuhamasisha wananchi hususan wafanyakazi wote kujitokeza kwa wingi kuja kuiadhimisha siku hiyo.

 “Ni wakati sahihi kwa wafanyakazi wote nchini kuitumia siku hii maalum katika kuiadhimisha na kuienzi ikiwa ni sherehe ya upekee sana hivyo mjitokeze kwa wingi pamoja na wananchi wote kwa ujumla.”Alisisitiza Nyamhokya.

Maadhimisho ya Sherehe za Mei Mosi yatahadhimishwa Kitaifa katika Mkoa wa Mbeya ambapo Mgeni Rasmi anatarajiwa kuwa Mhe.Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.John Pombe Magufuli, aidha maonesho hayo yatapambwa na shughuli mbalimbali ikiwemo; Maandamano ya wafanyakazi na magari, Kwaya maalum, Nyimbo maalum kutoka kwa Vyama vya Wafanyakazi, wimbo maalum kutoka kwa wasanii wa kizazi kipya, vikundi vya ngoma kutoka mikoa mbalimbali, Nyimbo maalum kutoka Jeshi la Kujenga Taifa (JKT).

Kauli mbiu ya maonesha ya mwaka huu inasema; “Tanzania ya Uchumi wa Kati Inawezekana, Wakati wa Mishahara na Masilahi Bora kwa Wafanyakazi ni SASA”


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527