KAMANDA MAMBOSASA AJIBU MASWALI YA JPM KUTEKWA MO DEWJI...."MIMI JUKUMU LANGU LILISHAKWISHA"


Siku chache baada ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt John Pombe Magufuli kuibua maswali juu ya tukio la kutekwa Mfanyabiashara Mohamed Dewji Kamanda wa Polisi Dar es salaam Lazaro Mambosasa amejitokeza na kusema yeye alishamaliza kazi yake.

Mambosasa amesema baada ya yeye kumaliza kazi yake alikabidhi kwa viongozi wake wa juu na kwa sasa wanaojua kinachoendelea ni Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) ambaye anatakiwa kutoa taarifa za uchunguzi zilizowasilishwa kwake.

Mambosasa amesema, “kuhusu maelekezo ya Rais aliyoyatoa kuhusu kutekwa kwa Mo, maadamu aliyatoa mbele ya Mkuu wetu wa Jeshi la Polisi na DCI ambao walikuwepo, jalada hilo lilishafika kwao, huko ndiko wanakojua kinachoendelea".

“Mimi jukumu langu lilishakwisha kwa hiyo ni suala la maamuzi ya juu kuhusu hatua zilizofikiwa kwenye jalada hilo", ameongeza Kamanda Mambosasa.

Mapema juzi Ikulu akiwaapisha Makamshna wa juu wa Jeshi la Polisi, Rais Magufuli alisema, "Jeshi la Polisi linatakiwa kuelewa kuwa Watanzania sio wajinga, kama suala la kutekwa kwa Mo Dewji linaacha maswali, tuliambiwa alitekwa na wazungu lakini lilipoisha haikueleweka, mwishoni aliyetekwa alionekana anakunywa chai na Mambosasa."

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527