MAKONDA : RUGE NI ZAIDI YA RAFIKI YANGU...NILIOMBA WANIONDOE KWENYE RATIBA

Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Paul Makonda amesema kwamba kutokana na uchungu alioupata wa kuondokewa na 'kaka' yake Ruge Mutahaba, alikosa hata cha kuzungumza kwa jamii, na kuitaka familia kumtoa kwenye ratiba ya kuongea.

Akizungumza kwenye tukio la kuaga mwili wa marehemu Ruge Mutahaba katika ukumbi wa Karimjee, Paul Makonda amesema kwamba alipata wakati mgumu sana kutokana na taarifa za kifo cha Ruge, hivyo walipomwambia yupo kwenye ratiba ya kutoa salam za rambi rambi, aliomba familia isimuweke kwani hana cha kuongea, na kufikia hatua ya kukesha akimuomba Mungu ampe neno la kuongea ambalo mpaka sasa hajajua aseme nini.

“Jana wakati tunajadiliana habari ya kutoa salamu za rambirambi, kwangu nilikuwa na wakati mgumu sana kwa sababu Ruge ni zaidi ya rafiki kwangu, na familia ilikuwa inajua, nikawa natafakari nasema nini mwishowe ikafika hatua nikawaambia niondoeni kwenye ratiba, kwa sababu tangu nilipopata taarifa za kumpoteza kaka yangu Ruge, sikupata nafasi ya kusema chochote kile, si kwa sababu nilikuwa sitaki, lakini niseme nini kwa ndugu yetu mpendwa, usiku kucha nilikuwa namuuliza Mungu naenda kusema nini”, amesema Paul Makonda.

Paul Makonda ameendelea kwa kusema kwamba........ “mpaka leo nimefika hapa asubuhi, sina cha kusema, nimemsihi sana Mungu nipatie hata neno moja la kusema, lakini Mungu bado hajanipa cha kusema, Mungu akinipa kibali cha kusema atanipa na cha kusema”.

Sambamba na hilo Paul Makonda amewaomba radhi wakazi wa Dar es salaam kwa usumbufu walioupata jana wakati wakitoka kupokea mwili uwanja wa ndege, na kusema kwamba alifanya hivyo ili kumpa heshima Ruge Mutahaba.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527