MBOWE NA VIGOGO WENGINE 13 KUPISHANA MAHAKAMA YA KISUTU KESHO

Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na vigogo wengine 13 kesho Alhamisi Januari 3, 2019 watafika katika mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kusikiliza kesi zinazowakabili.

Miongoni mwa kesi hizo ni za kufanya mikusanyiko isivyo halali inayowakabili viongozi tisa wa Chadema.

Kati ya vigogo hao wa Chadema, Mbowe na mhazini wa Baraza la Wanawake la chama hicho (Bawacha), Esther Matiko ndio wapo gerezani tangu Novemba 23, 2018 baada ya kufutiwa dhamana na hakimu mkazi mkuu wa mahakama hiyo, Wilbard Mashauri.

Washtakiwa wengine katika kesi hiyo ya jinai namba 112 ya 2018 ni mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa; mbunge wa Kibamba, John Mnyika; Katibu wa Chadema, Dk Vincent Mashinji na mbunge wa Bunda, Ester Bulaya.

Wengine ni naibu katibu mkuu wa Chadema-Zanzibar, Salum Mwalimu; mbunge wa Tarime Vijijini, John Heche na mbunge wa Kawe, Halima Mdee.

Kwa pamoja wanakabiliwa na mashitaka 13, ikiwemo kula njama, kufanya mkusanyiko wenye ghasia, kuhamasisha hisia za chuki, kushawishi hali ya kutoridhika, uchochezi na kushawishi utendaji wa kosa la jinai kati ya Februari Mosi na 16, 2018.

Kesho pia itasikilizwa kesi ya uhujumu uchumi inayomkabili Harbinder Seth na mfanyabiashara James Rugemalira.

Kesi nyingine itakayosikilizwa ni kesi ya mauaji ya aliyekuwa mjumbe wa tume ya mabadiliko ya Katiba, Dk Sengondo Mvungi.

Na Hadija Jumanne, Mwananchi 

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527