KIGWANGALLA AIVUNJA BODI YA UTALII (TTB)


Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk Hamis Kigwangalla amevunja bodi ya wakurugenzi ya Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) kuanzia jana Ijumaa na kutoa miezi mitatu kwa menejimenti kujirekebisha kinyume na hapo ataifumua.

Waziri huyo ametangaza kuunda bodi mpya ya wakurugenzi ambayo itakuwa na wajumbe vijana watakaokwenda na kasi katika kazi hiyo ya kutangaza vivutio.

Dk Kigwangalla amefikia uamuzi huo kwa kile alichoeleza kuwa TTB imeshindwa kutekeleza maelekezo yake yenye lengo la kutangaza vivutio vya utalii.

Akitoa uamuzi huo jana Ijumaa Januari 18, 2019 mbele ya waandishi wa habari Dk Kigwangalla ameeleza kutotangazwa kwa vivutio vya utalii kunaifanya Serikali inyooshewe kidole na kuonekana haifanyi kazi.

Amesema kwa kipindi cha mwaka mmoja ametoa maelekezo zaidi ya 15 lakini hayajafanyiwa kazi jambo linalosababisha yeye kutukanwa.

“Serikali ikitukanwa kwenye sekta ya maliasili na utalii maana yake natukanwa mimi naonekana sitoshi kwenye nafasi hii, “ amesema Dk Kigwangalla.

Miongoni mwa maelekezo ambayo hayajafanyiwa kaiz ni pamoja na TTB kutoweka mabango ya kutangaza utalii katika miji mikubwa ikiwemo Dar es Salaam kuanzia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA)

Jingine ni kushindwa kuwatumia watu maarufu na wasanii kutangaza vivutio vya utalii, kushindwa kutangaza vivutio kwenye michezo, kutotengenezwa kwa video na filamu fupi zinazojumuisha vivutio na nyingine nyingi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527