WABUNGE WA CCM WANAOTAFUTA KIKI KWA MGONGO WA JPM WAONYWA

Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM Taifa, Humphrey Polepole amewataka wabunge wa CCM nchini, kuacha kulala usingizi au kutafuta kiki ya kisiasa kwa mgongo wa Rais John Magufuli.


Badala yake, amewataka kuwatumikia wananchi katika majimbo yao na kuiga mfano uliofanywa na mbunge wa jimbo la Peramiho, Jenista Mhagama wa kujikita katika kusaidia ujenzi wa ofisi za matawi ya chama jimboni humo.

Polepole alitoa kauli hiyo juzi katika mkutano mkuu wa jimbo la Peramiho ambapo pia alikabidhi pikipiki 16 zenye thamani zaidi ya Sh milioni 45 kwa ajili ya makatibu kata wa chama hicho. 

Pia alikabidhi baiskeli 132 kwa ajili ya makatibu wa matawi, bati 835 kwa ajili ya ofisi za matawi na saruji mifuko 1,230 kwa ajili ya matawi hayo na ambavyo vilitolewa na Jenista alisema vifaa hivyo vitakuwa msaada mkubwa kwa viongozi wa kata na matawi katika kutekeleza majukumu yao.


Polepole alisema kuwa jukumu la viongozi wa kata na matawi ni kuhakikisha wanavitunza vifaa hivyo ambavyo ni mali ya chama na kwamba pasitokee kiongozi au mtendaji kutumia vibaya vifaa hivyo ambavyo vimetolewa na mbunge huyo wa jimbo la Peramiho. 

Kwa upande wake mbunge wa jimbo la Peramiho, Jenista Mhagama alisema katika jimbo hilo kulikuwa na matawi ambayo ofisi zake hazifanani na Chama Cha Mapinduzi ambacho ni kikongwe hapa nchini na duniani hivyo ameamua kwa dhati kusaidiana na wanachama kurekebisha hali hiyo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527