WAZIRI LUHAGA AKOMALIA 'OPERESHENI NZAGAMBA'..KAFICHUA NYAMA MBOVU

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina amesema Serikali haitakubali Tanzania kugeuzwa kuwa dampo la bidhaa za mifugo zilizokwisha muda wa matumizi na kuua uwekezaji kwa manufaa ya watu wachache.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Saalam juzi, wakati wa kutoa matokeo ya ‘Operesheni Nzagamba’ iliyoendeshwa kwa vipindi viwili tofauti, Waziri Mpina alisema kilo 26,295 za bidhaa za nyama na maziwa zimekamatwa,baada ya kuingizwa nchini kutoka nje bila vibali, kulipiwa ushuru wala kuhakikiwa ubora wake.

Pia kilo 2,376 za bidhaa za nyama na maziwa yaliyokwisha muda wa matumizi nazo zikikamatwa zikiuzwa maeneo mbalimbali na kuhatarisha afya za walaji na kuingia katika hatari ya kupata magonjwa makubwa ikiwemo saratani.

“Hatutakubali kuua uwekezaji, viwanda na ajira za Watanzania kwa manufaa ya watu wachache, hatutakubali kuziweka rehani afya za watanzania eti kwa sababu ya uwekezaji operesheni hizi zitaendelea hadi pale wahalifu hao watakapoacha mchezo huu mchafu,” alisema Mpina.

Alisema hivi karibuni kwenye mitandao ya kijamii kuliibuka taharuki juu ya hatua zinazochukuliwa na Serikali dhidi ya wahalifu katika operesheni inayoendelea katika maeneo mbalimbali nchini.

Alisema operesheni hiyo, inayoendeshwa kwa mujibu wa sheria ina lengo la kudhibiti uingizaji holela wa mazao ya mifugo nchini, kudhibiti uuzaji wa mazao ya mifugo, pembejeo na chakula cha mifugo kilichokwisha muda wa matumizi na utoroshaji wa mifugo na mazao yake nje ya nchi. 


Alisema kilo 17,712 za pembejeo za mifugo zilizokwisha muda wa matumizi zilikamatwa, huku kilo 880 za nyama na maziwa ambazo hazina lebo wala taarifa yoyote katika vifungashio pamoja na usajili kutoka mamlaka husika nazo zikikamatwa.

Alisema tani 25,423 za chakula cha mifugo zilikamatwa zikisafirishwa kwenda nje ya nchi bila vibali ambapo katika uhakiki wa hesabu za ulipaji ushuru kwa kampuni chache zilizofanyiwa uhakiki katika kipindi cha mwaka wa fedha 2017/18, ilibainika Sh bilioni 4.25 zilikwepwa kulipwa


Alisema ng’ombe 40,954, mbuzi na kondoo 165,115 nazo
zilikamatwa zikiwa zinatoroshwa kwenda nje ya nchi bila vibali na bila kulipa ushuru wa aina yoyote huku zaidi ya ng’ombe 50,000 zilikamatwa zikiwa zimeingia nchini bila vibali

Katika operesheni hiyo,vifaranga 21,100 na mayai 21,480 yalikamatwa yakiingia nchini bila vibali ambapo yalitaifi shwa na Serikali kisha kuketetezwa.

Alisema licha ya bidhaa zinazoingizwa nchini bila vibali na huku Tanzania ikiwa na mifugo mingi, uagizaji wa bidha za mifugo kutoka nje ya nchi ni mkubwa nchini ambapo uagizaji wa bidhaa za nyama nchini umefi kia thamani ya wastani wa sh. bilioni 10 huku maziwa ikiwa ni wastani wa sh bilioni 30 kwa mwaka.

Waziri Mpina ametaja baadhi ya madhara ya uingizaji holela wa bidhaa hizo nchini ikiwemo kuathiri afya za wananchi kunakoweza kusababisha maradhi sugu ikiwemo saratani.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527