SUMAYE AWACHONGANISHA CCM

Baraza Kuu la Chadema Kanda ya Pwani limetoa wito kwa serikali kuwachukulia hatua watu walioanzisha mchakato wa upatikanaji wa katiba mpya au wanaokwamisha mchakato huo, likidai kuwa uamuzi huo umepoteza fedha za umma.

Akitoa maazimio ya baraza hilo, leo tarehe 24 Desemba 2018 jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Chadema Kanda ya Pwani, Frederick Sumaye amesema kama mchakato huo ulioanzishwa na serikali ya CCM ya awamu ya nne haukuwa uamuzi sahihi, wahusika wachukuliwe hatua kwa ubadhirifu wa fedha za umma.

“Kama mchakato wa katiba ulioanzwa na serikali ya CCM ya awamu ya nne haukuwa uamuzi sahihi, wa serikali uliokuwa na Baraka za chama hicho tawala, sababu fedha zetu zimepoteza nyingi basi wahusika wachukuliwe hatua kwa ubadhirifu wa fedha za umma,” amesema Sumaye.

Katika hatua nyingine, Sumaye amesema kama mchakato huo ulikuwa halali na kupata baraka za CCM ,baraza hilo linaitaka CCM kuilazimisha serikali iliyopo madarakani kuuendeleza mchakato huo au kuwawajibisha wanaoukwamisha kwa kuwa fedha za umma zilizotumika katika mchakato huo zimepotea bila kuleta matokeo yaliyotarajiwa.

“Kama mchakato ulikuwa halali na wenye baraka za chama hicho tawala, basi watawala wa sasa ama chama chao kiwalazimishe kuendelea na mchakato wa katiba mpya au kiwashtaki na kuwawajibisha kwa ubadhirifu wa fedha za umma zilizopotea bila matokeo tarajiwa,” amesema Sumaye.

Sumaye ameeleza kuwa, kama mchakato huo ungefanikiwa, katiba mpya ingepatikana na kutoa mchakato mzuri kuelekea uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwaka 2020.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527