NIKKI WA PILI ATAJA FURSA ,MAKTABA MPYA YA UDSM


Msanii wa muziki wa HipHop nchini anayewakilisha kundi la Weusi, Nikki wa Pili amezitaja fursa ambazo zinaweza kutumiwa na watanzania katika maktaba mpya ya Chuo Kikuu cha Dar es salaam (UDSM) ili kuweza kujiongezea maarifa.

Nikki ameyasema hayo baada ya Rais John Magufuli kuzindua maktaba hiyo ambayo ni ya kwanza katika ukanda wa Afrika Mashariki na kati, Nikki amesema kuwa vijana wanapaswa waitumie fursa hiyo ili waweze kukuza uwezo wao wa kujieleza na kuwasilisha mawazo yao kwa njia sahihi.

Katika ukurasa wake wa Twitter, Nikki ameandika, "maktaba ya kuchukua wasomaji 2100, ina maana ni fursa kila siku kwa vijana 21,000 kujivunia maarifa. Itumieni sana, itumieni vizuri ili kujenga uwezo wa kujieleza, kupanga mawazo, kutafuta ukweli na kuuwakilisha, ni silaha adhimu katika pori la Maisha. Maktaba ni uhai wa jamii".

Licha ya kuwa ni maktaba kubwa katika ukanda wa Afrika Mashariki, sifa nyingine za maktaba hiyo ni uwezo wa kuhudumia wasomaji 2,100 kwa wakati mmoja pamoja na kuwa na ukumbi wa mikutano wenye uwezo wa kuchukua watu 600.

Pia ina uwezo wa kutunza zaidi ya vitabu 400,000. Akitoa maelezo ya awali kabla ya uzinduzi rasmi wa maktaba hiyo, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam, Prof. Anangisye amesema kuwa watu mabalimbali hata ambao si wanafunzi wataruhusiwa kutumia maktaba hiyo katika kujiongezea maarifa.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527