CHARLES MWIJAGE ACHEKELEA KUTUMBULIWA NA JPM

Aliyekuwa Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage amezungumzia hatua ya Rais John Magufuli kumwengua kwenye wadhifa wake akisema anakuwa mzuri anapotokea benchi.


Amesema hayo leo Novemba 12, 2018 Ikulu jijini Dar es Salaam, mara baada ya kuapishwa mawaziri wawili na manaibu waziri wanne akiwamo anayechukua nafasi yake Joseph Kakunda.


“Mimi wanaonijua, wanafahamu kazi yangu, nikiwa benchi ninakuwa mzuri zaidi, mimi ndiyo nilishiriki kubadilisha sera ya mafuta na tozo ya Rea ambapo Serikali ilikuwa inapoteza bilioni 600,” amesema Mwijage.


Mwijage amesema waziri yeyote wakiwamo hao walioteuliwa akitaka ushirikiano yupo tayari kufanya hivyo, na kuongeza kuwa kitu anachokumbuka na alichokiacha kama alama ni kuwaelewesha Watanzania kuhusu dhamira ya kuwa na nchi ya viwanda, ambapo hivi sasa nchi nzima wanazungumza viwanda.


“Ilikuwa kazi ngumu na nisiyoweza kuisahau, kuwaeleza Watanzania hadi waelewe viwanda ni nini na wanatakiwa kufanya nini, kwa sababu wengi walikuwa na mawazo ya kuwa na mitambo mikubwa, mashine nyingi, lakini niliwaambia hata ukiwa nazo cherehani nne kama alizokuwa nazo A to Z unaweza kuanzisha kiwanda na baadaye kikakua,” ameongeza.


Awali Rais Dkt John Pombe Magufuli ametaja sababu ya kuwatumbua waliokuwa Mawaziri wa Kilimo, Dkt Charles Tizeba, pamoja na Waziri wa Viwanda na Biashara Charles Mwijage kuwa walishindwa kumaliza mgogoro wa zao la korosho, huku akiwapongeza kwa kuhudhuria hafla ya uapisho.


"Kwa dhati kabisa nawapongeza aliyekuwa Waziri Charles Tizeba na Charles Mwijage kuja kushuhudia kuapishwa kwa wenzao, huu ni moyo wa kiungwana", amesema Rais Magufuli.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527