BWANA HARUSI KADA WA CCM AFARIKI SIKU MOJA KABLA YA KUFUNGA NDOA


Mkazi wa Mbaramo, Muheza mkoani Tanga, Hatibu Ally, amefariki dunia ghafla siku moja kabla ya kufunga ndoa. 

Ally alitarajiwa kufunga ndoa na mchumba wake aliyefahamika kwa jina la Asha Salim na kifo chake kimeacha gumzo kwa wakazi wa eneo hilo wakiwamo ndugu zake na wa mchumba wake.


Kifo cha bwana harusi huyo mtarajiwa ambaye alikuwa kamanda wa kikosi cha CCM, maarufu kama Green Guard, kilitokea usiku wa kuamkia juzi na kwamba alitarajiwa kufunga ndoa juzi. 

Dada wa bibi harusi, Mwanjaa Salim, alisema ndoa hiyo kati ya Ally na Asha ilikuwa ifungwe juzi na maandalizi yote yalikuwa yamekamilika.

Alisema Jumatano wiki hii walimpeleka mdogo wake kwa kungwi waliyemtaja kwa jina la Hadija Awadhi kijijini Ngwaru ikiwa sehemu ya maandalizi ya ndoa hiyo, ambayo haijafungwa kutokana na kifo cha bwana harusi mtarajiwa. 

Kwa mujibu wa Mwanjaa, Jumatano jioni bwana harusi alikwenda kwenye mazoezi ya mpira katika Uwanja wa Jitegemee na wenzake na kwamba majira ya saa moja usiku walirudi nyumbani akiwa na afya njema. 

Alisema Ally alifika nyumbani kwake akaoga maji kisha alitoka tena kwenda kwa rafiki yake ndipo huko alianza kusikia baridi ya homa na kisha kuanza kutapika mapovu mdomoni.Alisema bwana harusi huyo baada ya kuzidiwa alipelekwa na wenzake katika kituo cha Afya cha Ubwari kwa matibabu na baadae alihamishwa Hospitali Teule ya Wilaya ya Muheza kwa matibabu.

Hata hivyo, alisema Ally alipoteza maisha, hatua ambayo ilisababisha taharuki katika familia zote huku mama wa bibi harusi akizimia kutokana na shinikizo la damu baada ya kusikia mkwewe mtarajiwa amefariki dunia. 

Salma Salim, dada mwingine wa bibi harusi, alisema msiba wa Ally ulifanyika nyumbani kwa wazazi wake, Michungwani wilayani hapa na kuzikwa na mamia ya wananchi, wakiwamo viongozi wa chama na serikali wilayani Muheza.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527