ENGLAND WARUDIA REKODI YAO YA MWAKA 1990...IMEPOKEA KICHAPO


Kikosi cha timu ya taifa ya England

Timu ya taifa ya England imepoteza mchezo wa kutafuta mshindi wa tatu kwenye fainali za kombe la dunia kwa mara ya pili, baada ya leo kukubali kichapo cha mabao 2-0 kutoka kwa timu ya taifa ya Ubelgiji.

Mara ya mwisho England kufika hatua hii ilikuwa mwaka 1990, ambapo ilipoteza katika mchezo wa kumsaka mshindi wa tatu baada ya kufungwa na Italia mabao 2-1. Hivyo leo imerudia tena historia hiyo kupitia mabao ya Thomas Meunier na Eden Hazard.

Kwa upande wa Ubelgiji ikiwa na kizazi cha dhahabu chenye majina kama Hazard, De Bruyne, Lukaku, Kompany na Courtois wamefanikiwa kupata nafasi ya juu zaidi katika historia ya taifa hilo kwenye kombe la dunia ambayo ni kumaliza katika nafasi tatu.

Kikosi cha timu ya taifa ya Ubelgiji.

Baada ya kupoteza mechi ya nusu fainali dhidi ya Croatia na leo dhidi ya Ubelgiji, England sasa imepoteza mechi mbili mfululizo kwa mara ya kwanza tangu mwaka 2014 ilipofungwa na Italia pamoja na Uruguay katika mechi za fainali za kombe la dunia nchini Brazil.

Mchezaji Eden Hazard wa Chelsea na Ubelgiji ameifikia rekodi ya nyota wa zamani wa taifa hilo Jan Ceulemans ya kuhusika kwenye mabao 7 katika fainali za kombe la dunia. Hazard amefunga mabao 3 na kusaidia mengine manne.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527