MWANAMKE AUAWA KWA KUKATWA SHOKA KISHAPU - SHINYANGA

Kamanda wa jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga ACP Simon Haule 
***
Mwanamke aliyejulikana kwa jina la Nyawamba Dohoi (61) mkazi wa kitongoji cha Kiloleli kijiji cha Ilebelebe kata ya Itilima wilayani Kishapu mkoa wa Shinyanga ameuawa kwa kukatwa na kitu kinachodhaniwa kuwa ni shoka/panga maeneo ya kichwani na mikono yote na watu wasiojulikana.

Akielezea kuhusu tukio hilo, ndugu wa marehemu Sia Shija ambaye ni wifi yake amesema kuwa waligundua kuuawa kwa marehemu Dohoi jana Julai 11,2018 majira ya saa tatu asubuhi baada ya jirani mmoja kwenda katika mji huo kumuulizia na kuchukua ndoo yake aliyokuwa ameiazima.

Shija alisema kuwa marehemu Dohoi (mjane) aliuawa akiwa katika chumba chake akiwa amelala na wajukuu zake wawili na kwamba hafahamu watu waliohusika na unyama huo.

Mwenyekiti wa kijiji hicho Thomas Nkindo amesema kutokana na mauaji hayo wananchi wengi wamekimbia makazi yao kwa hofu ya kukamatwa na polisi.

Kamanda wa jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga ACP Simon Haule amesema chanzo cha mauaji hayo ni kuwania mali alizoachiwa marehemu huyo na mume wake ambaye  pia ni marehemu.

Amesema jeshi la polisi linamshikilia mtoto wa marehemu Ngassa Mathias (24) kwa maelezo zaidi juu ya uchunguzi zaidi wa tukio hilo.
Na Mwandishi wa Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527