MUME AUA MKE KWA RUNGU AKIMTUHUMU KUZAA WATOTO WA KIKE TU


Na Rhoda Ezekiel - Malunde1 blog Kigoma 

Mwanamke mmoja aliyefahamika kwa jina la Selina Simon (35) mkazi wa Kijiji cha Itumbiko Wilayani Kakonko,ameuawa kwa kupigwa rungu na fimbo sehemu mbalimbali za mwili wake ikiwemo kichwani na mume wake Ndimugwanko Mlovezi (30) mkazi wa Itumbiko aliyemtuhumu kwanini anazaa watoto wa kike tu.

Malunde1 blog imeambiwa kuwa mwanamke huyo amefariki dunia Aprili 20,2018 majira ya saa moja na nusu usiku na kuacha mtoto mchanga.

Akizungumza baada ya kufika nyumbani kwa marehemu huyo Mkuu wa wilaya ya Kakonko Kanali Hosea Ndagala amesema kwa mujibu wa ndugu wa marehemu huyo wanadai alipigwa na mume wake akawa anaogopa kusema kilichomkuta  na baada ya siku mbili alizidiwa na kumwambia mama yake kuwa amepigwa.

Ameeleza kuwa baada ya kupelekwa hospitali, tarehe 20 Aprili mwaka huu alifariki dunia kutokana na maumivu aliyokuwa nayo baada ya kupigwa.

Kanali Ndagala amesema chanzo cha tukio hilo ni migogoro ya familia ambapo inasadikika mtuhumiwa alikuwa akimtuhumu marehemu kuzaa watoto wa kike tu na kusababisha kuanza kumpiga.

 Kamanda wa jeshi la polisi mkoani Kigoma, Maltin Otieno amethibitisha kutokea kwa tukio hulo na kwamba  mtuhumiwa huyo anashikiliwa na jeshi la polisi kwa kosa la mauaji na atafikishwa mahakamani.

Aidha ametoa wito kwa wananchi kuacha kujichukulia sheria mkononi na kutenda vitendo vya ukatili kwakuwa ni kisa kisheria.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527